October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TBL Plc kushiriki siku 16 za maadhimisho ya kupinga ukatili

Na Irene Clemence,TimesMajira Online,Dar es Salaam

KAMPUNI ya Bia ya Tanzania (TBL Plc) itaungana na wadau wengine katika mapambano dhidi ya vitendo vya ukatili wa Kijinsia (GBV) wakati wa siku 16 za maadhimisho hayo kupitia kampeni yake ya #IsiweSababu.

Maadhimisho ya siku 16 za kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia huadhimishwa kimataifa kila mwaka kuanzia Novemba 25 hadi Desemba 10 ambayo ni siku ya Haki za Binadamu.

Mkurugenzi Mtendaji wa TBL Plc,Philip Redman

Nchini Tanzania maadhimisho hayo hushirikisha pamoja mtandao wa mashirika, katika kupiga vita vitendo vya Ukatili wa Kijinsia Nchini.

Mkurugenzi Mtendaji wa TBL Plc,Philip Redman amesema, “kwa miaka 3 iliyopita kampuni yetu imeadhimisha siku 16 za kupinga vitendo vya unyanyasaji na ukatili wa kijinsia kupitia kampeni yake ya #IsiweSababu.

Kampuni imefanya kazi na wahusika mbalimbali kuunda jukwaa ambalo limeweza na limedhamiria: Kubadilisha dhana kuwa pombe ni kisingizio cha unyanyasaji na changamoto za kimaadili za kijamii; kubuni na kueneza elimu juu ya Ukatili wa Kijinsia (GBV); Kuchochea mazungumzo ambayo yanakuza uhusiano mzuri; Kutoa elimu kwa watu yanayohusiana mabadiliko mazuri ya tabia.

Ameendelea kusema “Mwaka huu tofauti na miaka mingine, tumejitolea kutumia njia za kidigitali ambapo tutaendesha mijadala na kutoa elimu kwenye jamii kuwa pombe sio sababu ya kufanya vitendo vya ukatili wa kijinsia. Watu wanapaswa kuelewa kuwa Pombe sio kisingizio cha kufanya vitendo vya unyanyasaji na ukatili wa kijinsia ”.

TBL inaamini kuwa vitendo vya ukatili wa kijinsia vinaweza kukomeshwa nchini ikiwa jamii nzima kwa kushirikiana na serikali na vyombo vingine vya maamuzi watashirikiana kupaza sauti na kuchukua hatua dhidi ya ukatili wa kijinsia. Kampuni hiyo pia inatamani kujenga mazingira ambayo wanapenda kufanya kazi na kustawi.