October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali yaanzisha Kanda Mpya ya NFRA Songwe

Na Joyce Kasiki, TimesMajira Online, Dodoma

SERIKALI imeanzisha Kanda ya Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) katika Mkoa wa Songwe kutokana na uzalishaji wa mazao ya chakula katika mkoa huo kwa mwaka 2018/19.

Waziri wa Kilimo, Japhet Hasunga amesema kanda hiyo ilianzishwa rasmi Julai Mosi mwaka huu huku ikitarajia kuhudumia Mikoa ya Mbeya na Songwe.

“Kuanzishwa kwa kanda hii kumetokana na hali ya uzalishaji mkubwa wa chakula katika mikoa ya Songwe na Mbeya, pamoja na kujengwa kwa maghala na Vihenge vya Kisasa ambavyo vitaongeza uwezo wa uhifadhi kutoka tani 17,000 za awali hadi kufikia tani 37,000,” amesema Hasunga.

Katika kituo cha Vwawa, zoezi la ununuzi wa mahindi lilianza rasmi Julai 6, mwaka huu ambapo kwa sasa Serikali inaanza na ununuzi wa tani 10,000 na inanunua kwa bei ya shilingi 550 kwa kilo.

Hata hivyo Waziri huyo amesema, Wizara yake itaendelea kuongeza kiasi cha ununuzi kadri itakavyopata fedha kutoka serikalini huku akisema kuwa mtu yeyote anaruhusiwa kuuza mahindi NFRA bila kujali upendeleo wowote ili mradi mahindi hayo yawe na ubora unaotakiwa.

Katika taarifa hiyo pia amezungumzia kuhusu maonyesho ya wakulima na wafugaji (NaneNane) mwaka ambapo amezitaka taasisi na ,Wizara Mshirika,sekta binafsi na wadu wote kujitokeza kwa wingi kushiriki kwenye maonyesho hayo huku Serikali yaanzisha Kanda ya NFRA.

Amesema, katika maonesho ya mwaka huu, taasisi, Wizara, Mashirika, Sekta binafsi na wadau wote kujitokeza kwa wingi kushiriki kwenye maonesho hayo huku wakitumia ubunifu katika kutoa elimu na kuonyesha teknolojia zinazokidhi mahitaji ya wazalishaji na walaji wa bidhaa zinazozalishwa hapa nchini.

Waziri Hasunga amesema, lengo la maonesho hayo ni kutoa fursa kwa wakulima, wafugaji, wavuvi na wanaushirika kuona na kujifunza matumizi ya teknolojia bora za kilimo, uvuvi, ufugaji kwa ajili ya kuongeza tika katika uzalishaji kwa uhakika wa chakula,kukidhi mahitaji ya viwanda na masoko ya ndani na nje ya nchi.

“Kwa maana hiyo kuna kila sababu ya kuwa wabunifu kwa kutoa elimu kwa makundi hayo yote ili yajue namna bora ya uzalishaji wenye tija ya kuitosha,” amesema Waziri Hasunga

Amesema, maonesho yatafanyika katika Kanda nane nchini huku akitoa wito kwa wadau wote wa sekta ya umma na binafsi kukamilisha maandalizi ya kushiriki katiika viwanja vya maonesho vilivyopo kwenye kanda hizo .

Kauli mbiu ya mwaka huu katika maonesho hayo ni kwa maendeleo ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Chagua Viongozi bora 2020’ huku ambapo amesema kaulimbiu hiyo inalenga kutoa hamasa kwa wananchi kuchagua viongozi bora watakaokuwa chachu ya kuleta mapinduzi kwa ajili ya maendeleo ya sekta ya kilimo ili kuinua ustawi wa maisha ya wakulima, wafugaji na wavuvi nchi.