June 30, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali yaahidi kushirikiana na MCB

Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online

Serikali imeahidi kushirikiana kwa karibu na Benki ya Biashara ya Mwalimu (MCB) ili kusaidia kuondoa changamoto ndogondogo zinazoikabili benki hiyo ili iongeze ufanisi wake katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Hayo yamesemwa na Mstahiki Meya wa Manispaa ya Iringa Bw. Ibrahim Ngwada, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (TAMISEMI) kwenye Mkutano Mkuu wa Nane wa MCB huku akibainisha kuwa benki hiyo ina nafasi ya kutumia fursa mbalimbali za uwekezaji ikiwemo Utali, Afya na Michezo katika Mkoa wa Iringa ili kuendelea kujiongezea wanachama.

Amesema Serikali inatamani kuona ukuaji mkubwa wa sekta ya fedha kwa ujumla, na kwamba uimara wa benki kama ya Mwalimu utasaidia sana kukuza uchumi wananchi na Mwananchi mmoja mmoja.

Mstahiki Meya wa Manispaa ya Iringa Ibrahim Ngwada amesema wanahisa wakuu wa benki hiyo ni Chama cha Walimu (CWT), Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (PSSSF), na Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF), ambao wanamiliki asilimia 16.2 TTU hisa 12.95, TDCL 3.2. Aidha, wanahisa walimu mmoja mmoja wanamiliki asilimia 35, na wanahisa wengine mbalimbali wanamiliki asilimia 16.

Hii inaonesha kuwa benki hii ni jumuishi katika umiliki na huduma zake, ikiwakilisha malengo ya serikali ya kufanikisha ushiriki na umiliki wa shughuli za kiuchumi kwa wananchi.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi, Francis Ramadhani, amezishukuru taasisi zinazosimamia sekta ya fedha, yaani Benki Kuu ya Tanzania (BOT), Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), pamoja na serikali kuu chini ya uongozi wa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa miongozo iliyosaidia benki kuzidi kujiimarisha.

Katika mazingira ya sasa ambapo vitendo vya wizi wa fedha kwa njia ya mtandao vinaongezeka, Mwalimu Commercial Bank Plc. (MCB) imechukua hatua madhubuti kuhakikisha usalama wa amana za wateja wake.

Bw. Francis Ramadhani, alisema safari ya benki hiyo iliyoanza 2016 baada ya kupata leseni toka Benki Kuu ya Tanzania, imekuwa ni safari nzito lakini yenye mwelekeo chanya na akauhakikishia umma wa Watanzania kuendelea kuiamini kwa kuwa sasa imetoka kwenye kupata hasara na kuanza kutengeneza faida.

Amesema benki hii ni ya Watazania wote, huku wabia wake wakubwa wakiwa ni PSSF na NHIF pamoja na wali, lakini watanzania wa kada zote wameitwa kunifaifa na MCB.

Naye, Afisa Mtendaji Mkuu wa MCB, Richard Louis Makungwa, alieleza kuwa benki hiyo inaendeshwa kwa takriban asilimia 95 kidigitali, na kwamba mfumo wake wa kudhibiti uhalifu na wizi wa mtandao ni wa kisasa, ukisimamiwa na idara maalumu.

Afisa Mtendaji Mkuu wa MCB, Bw. Richard Louis Makungwa, ameeleza kuwa benki hiyo inaendeshwa kwa takriban asilimia 95 kidigitali, na kwa msingi huo, mfumo wake wa kudhibiti uhalifu na wizi wa mtandao ni wa kisasa, ukisimamiwa na idara maalumu ili kuhakikisha fedha za wateja wake ziko salama wakati wote.

Makungwa alieleza hayo muda mfupi kabla ya kuanza kwa mkutano wa wanahisa uliofanyika mjini Iringa, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.

Aliuhakikishia umma wa Watanzania kuwa MCB imejiimarisha kiufundi na kinyenzo, na inatekeleza mkakati wa usalama wa fedha kwa kutumia teknolojia ya kisasa.

“Tunatumia teknolojia za hali ya juu kuhakikisha usalama wa miamala ya wateja wetu. Idara yetu maalum ya usalama wa mtandao inafuatilia na kusimamia mifumo yetu kwa umakini mkubwa ili kuhakikisha kwamba uhalifu wa mtandao unazuiwa kabla ya kutokea,” alisema Makungwa.

Maelekezo ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) yameongeza msukumo kwa mabenki nchini kuchukua hatua za haraka na za kina katika kuimarisha usalama wa kifedha, inaelezwa kuwa Benki Kuu ya Tanzania (BOT) ilitoa mwongozo wa kuzingatia matumizi ya teknolojia za kisasa kama vile encryption na multi-factor authentication, pamoja na kufanyia majaribio ya usalama wa mifumo ya ndani mara kwa mara, jambo ambalo MCB, wanaonekana kuliwekea mkakati mzito na kulitekeleza kwa vitendo .

Aidha, BoT ilisisitiza umuhimu wa kutoa elimu kwa wateja kuhusu jinsi ya kujilinda dhidi ya ulaghai wa mtandaoni.

Akizungumzia mwongozo huu wa Benki Kuu, Makungwa alisema, “MCB imekuwa mstari wa mbele katika kufuata maelekezo ya BoT, tumetekeleza hatua zote zilizopendekezwa na tumeongeza hatua za ziada kuhakikisha usalama wa fedha za wateja wetu.

“Tunafahamu kuwa uaminifu wa wateja wetu ni muhimu sana, na ndiyo sababu tunawekeza sana katika mifumo ya usalama wa mtandao.” Alisema Makungwa.


Mwalimu Commercial Bank Plc. imeendelea kupiga hatua za mafanikio katika nyanja mbalimbali, ikiwemo benki kupata faida baada ya kodi kwa mwaka wa fedha unaoishia Desemba 31, 2023.

Mafanikio haya yanatokana na uchumi wa dunia kuanza kuimarika mwaka 2023, pamoja na changamoto za kuyumba kwa soko la nishati na chakula, ukuaji dhaifu wa biashara, na hali ngumu ya kifedha kama ilivyoainishwa kwenye ripoti ya uchumi ya nchi robo ya mwaka inayoishia Septemba 2023 (Vol.Lv.No.3) ya Benki Kuu ya Tanzania.

Akitoa tathmini ya uendeshaji wa MCB mbele ya wanahisa kwenye mkutano wa nane mjini hapa, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi, Francis C. Ramadhani, alisema benki yao imeendelea kuwa imara ikikabili changamoto kadhaa.

Benki ilipata faida baada ya kodi ya shilingi milioni 11, ukilinganisha na hasara baada ya kodi ya shilingi milioni 331 iliyopatikana katika kipindi cha mwaka 2022, mafanikio haya yamechangiwa na ongezeko la mapato ya jumla kwa asilimia tatu.

Ramadhani alisisitiza kuwa mapato ya riba yaliongezeka kwa asilimia 20, ongezeko lililochangiwa kwa sehemu kubwa na uwekezaji katika mikopo ya muda mrefu kwa wateja wa mikopo wa muda mfupi, huku mapato yasiyo na riba yakiongezeka kwa asilimia 3.

Kitabu cha amana za wateja kiliongezeka kwa asilimia moja licha ya changamoto za ukwasi. Benki ilifunga mwaka ikiwa na matawi mawili yanayotoa huduma, yote yakiwa jijini Dar es Salaam, na ofisi nane za kanda zinazotoa huduma katika mikoa ya Morogoro, Mwanza, Mbeya, Dodoma, Arusha, Kigoma, Rukwa na Mtwara.