October 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Sekta ya Madini sasa inachangia asilimia 5.2

Na Judith Ferdinand, TimesMajira Online, Mwanza

IMEELEZWA kuwa kwa sasa sekta ya madini inachangia pato la taifa kwa asilimia 5.2 huku malengo ikiwa Ni kufikia asilimia 10 kabla ya mwaka 2025,kwa kasi ile ile ilioingiza Tanzania uchumi wa kati kabla ya muda.

Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa Chama cha Wanajiosayansi Tanzania(TGS),Kamishina Tume ya Madini Professa Abdulkarim Mruma wakati wa ufunguzi wa mkutano mkuu uliombatana na warsha ya kitaaluma ya Wanajiosayansi kwa mwaka 2020 uliofanyika jijini Mwanza.

Amesema kwa mujibu wa takwimu za Time ya Madini na sekta ya madini kwa sasa inachangia asilimia 5.2 ya pato la taifa.

Hivyo kiwango hicho ni kikubwa ukilinganisha na asimilia 3.5 mwaka 2012 na asilimia 3.3 kwa mwaka 2011, hivyo kuongezeka kwa mapato ni kiashiria kuwa mchango wa sekta ya madini katika pato la taifa unaongezeka kwa kasi na ni dhahiri kwamba inaweza kufikia asimilia 10 kabla ya mwaka 2025.

Baadhi ya washiriki wa Mkutano Mkuu uliombatana na warsha ya kitaaluma ya Wanajiosayansi kwa mwaka 2020 uliofanyika jijini Mwanza. Picha na Judith Ferdinand

“Juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano,zimeonesha dunia kuwa Tanzania umeweka dhamira ya kweli ya kusimamia rasilimali za madini,ili kuhakisha kuwa nchi na watu wake wananufaika ipasavyo ni imani hii tunaona asilimia 10 ya mchango wa sekta ya madini katika pato la taifa utafanikiwa ifikapo 2025,”amesema Pro.Mruma.

Amesema,katika kushiriki kikamilifi katika maendeleo ya sekta ya madini nchini TGS kwa kutumia wataalamu wake waneanzisha programu maalumu ya kuwaendeleza wachimbaji wadogo ambao utaanza kwa kuwapatia mafunzo mbalimbali katika mkutano huo ambayo ni mwanzo na wamepanga kuwafuata popote walipo.

Amesema pia kuwapa huduma nyingine za kitaalamu zinazohitajika na wanafanya kazi kwa karibu na wizara husika pamoja na Tume ya Madini kwa kushirikiana na Jumuiya za Wachimbaji Wadogo(FEMATA na TAWOMA).

” Mfano mzuri wa kutumia utaalamu wetu katika uchimbaji mdogo ni mafanikio ya hivi karibuni ya bilionea Saniniu Laizer huko Mererani ambapo alimtumia mjiolojia mwenzetu Faustus Rutahindurwa ambapo alipata madini ya Tanzanite kilogramu 6.3 yenye thamani ya bilioni 4.9,ambaye amekiri jinsi utaalamu wa jiolojia ulivyomsaidia katika kufikia mafanikio yake hivyo ndugu Hawa wawili tumeona kuwatambua kipekee kwa kuwakabidhi tuzo ili kuweka alama kwa mafanikio walioyaleta,”amesema.

Pia alitumia fursa hiyo,kuwaomba wataalamu wa ujenzi kuwatumia wanajiolojia katika shughuli zao za ujenzi kwani hutumika kutoa ushauri wa kujua maeneo yenye miamba bora inayoweza kuhilmili ujenzi imara wa miundombinu mbalimbali pamoja na malighafi bora za kujengea miundombinu hiyo.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania(TPDC) James Mataragio amesema katika kufikia malengo waliojiwekea katika utafutaji wa mafuta na gesi ni lazima ipate
ushirikiano wa kutosha kwa wajiolojia kutoka kwenye taasisi mbalimbali hapa nchini,hivyo basi aliiomba kuendeleza ushirikiano ili kuifikisha Tanzania katika
kilele cha mafanikio ambacho wanayatamani.

“Hadi sasa mteja mkubwa wa gesi asilia ni TANESCO,ambapo asilimia 60 ya umeme unaozalishwa katika gridi ya taifa unatokana na gesi asilia,nafahamu kuwa jambo hili sio wengi wanaolifahamu lakini ndio ukweli ulivyo.

“Mbali na kuzalisha umeme, gesi asilia pia inatumika katika viwanda vipatavyo 48 hapa nchini, nyumba takribani 500 na magari zaidi ya 400 katika eneo la usambazaji gesi asilia TPDC tumejipanga pia kuongeza matumizi ya gesi asilia kwa kutekeleza miradi ya CNG lengo likiwa kuwafikia wateja walioko mbali na miundombinu ya gesi asilia,” amesema Mataragio.

Naye Mkurugenzi wa Masoko wa Kampuni ya Global Fortune Samuel Kisaro ambao kupitia Kampuni hiyo alimkabidhi hati ya kiwanja mjiolojia Faustus Rutahindurwa ambaye kupitia taaluma yake amefanikisha bilionea Saniniu Laizer huko Mirerani kufanikisha kupata madini ya Tanzanite,amesema wamemkabidhi kiwanja hicho ikiwa ni sehemu ya kutambua mchango wake kwa taifa.

“Tumeamua kumzawadia kiwanja cha makazi jijini Dodoma
kilichopo pembezoni mwa Wizara ya Madini ikiwa kama alama ya kuthamini Mchango wa wanajiolojia na wake binafsi katika taifa kwani tunaamini kuputia utaalamu wake bilionea Laizer ameweza kupata madini ambayo yatauzwa na fedha zitakazopatina zitasaidia katika kujenga barabara kupitia kodi na kusaidia vitu vingi katika jamii,hata sisi kwa namna moja tunefaidika kupitia utaalamu wake na ndio maana tumemzawadia kiwanja ili naye atukumbuke,”amesema Kisaro.

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza John Mongella,aliyekuwa mgeni rasmi katika mkutano huo,amesema kauli mbiu ya mkutano huo ‘ uongozi bora,utaalamu na weledi ,vichocheo vya maendeleo endelevu ya sekta ya madini nchini’, imekuja wakati muafaka wa kuchangiza maendeleo ya sekta hiy

Amesena inawakumbusha kuzingatia uongozi bora na kutumia utaalamu wao kwa weledi pamoja na kuzingatia maadili.