October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

REGROW yawa neema kwa wananchi wa Manienga,Mbarali

Na Mwandishi wetu,Timesmajira

Wakazi wa Kijiji cha Manienga Kata ya Mawindi Wilaya ya Mbarali Mkoani Mbeya ambao wanaojishughulisha na ufugaji pamoja na Kilimo wameishukuru serikali kwa kuwajengea mabirika ya kunyweshea mifugo pamoja na visima ambavyo vinawasaidia kupata huduma ya Maji safi na salama kwa sasa.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Manienga,Laison Mbende amesema kuwa kwa sasa mifugo inapata sehemu nzuri ya kunywea Maji lakini pia wanaendesha Kilimo vema mara baada ya vyanzo vya Maji kurekebishwa ambapo mara baada ya kumaliza kuyatumia Maji hayo kutoka Mto Kyoga huyaelekeza kwenda kwenye Mto Ruaha Mkuu kwa ajili ya Ikolojia ya Hifadhi ya Taifa Ruaha.

“Tunaishuku serikali ya awamu ya sita chini Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuruhusu Fedha za mradi wa REGROW kuletwa kuchimba visima, kurejesha mikondo ya mito iliyokuwa imeziba ambapo kwa sasa tunapata maji ya uhakika, pamoja na kutujengea Mabirika ya kunyweshea mifugo Maji ambayo yanatusaidia sana katika kitongoji chetu cha Chabegenja”-Ameeleza Mbende.

Aidha wananchi hao wameahidi kuitunza miundombinu hiyo ili fedha zilizowekezwa kukamilisha ujenzi wa Mabirika pamoja na uboreshaji vyanzo vya Maji katika mito iliyokuwa imepoteza kingo zake una kuwa na tija kwao na taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake Afisa Maji Kidakio cha Mto Great Ruaha,Abisai Chilunda ameeleza kuwa kupitia mradi wa REGROW wameweza kupanda miti takribani laki Moja na Sabini ambayo ni rafiki katika vyanzo vya Maji, ujenzi wa Mabirika matano ya kunyweshea mifugo, urejeshaji mito iliyopoteza mikondo ili kutiririsha Maji katika Mto Ruaha Mkuu kwa ajili ya uendelezaji hifadhi ya Taifa Ruaha pamoja na ujenzi wa Ofisi 10 za watumia wa Bonde la Usangu.