September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mkuu wa Mkoa wa Tabora Dkt. Philemon Sengati

RC Tabora aagiza kutengwa maeneo ya uwekezaji kilimo cha korosho

Na Tiganya Vincent, TimesMajira Oline,Tabora

MKUU wa Mkoa wa Tabora Dkt. Philemon Sengati ameziagiza Halmashauri zote kutenga maeneo makubwa kwa ajili ya uwekezaji wa kilimo cha korosho.

Mkuu wa Mkoa wa Tabora Dkt. Philemon Sengati

Ametoa agizo hilo wakati wa ziara yake ya kukagua shamba darasa la mkulima wa korosho katika Manispaa ya Tabora na alipokagua shamba la uzalishaji wa mbegu za korosho katika Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania Tawi la Tumbi.

Dkt.Sengati amesema Mkoa wa Tabora unalo eneo kubwa ni vema wakazi wake wakatumia fursa hiyo katika kulima korosho kwa wingi kwa ajili ya kuinua uchumi wa eneo hilo.

Amesema utafiti umeonyesha kuwa korosho katika Mkoa huo inaweza kuzaa mara mbili kwa mwaka ukilinganisha na maeneo mengine hapa nchini na hivyo kuwa chanzo kikubwa cha mapato kwa wananchi.

Dkt.Sengati amesema lengo la Mkoa ni kuongeza korosho kama zao la kimkakati kwa kulima kwa wingi ili liweze kupeleka mbele uchumi wa Mkoa ambao utawawezesha wakazi wengi kujenga nyumba bora, kula chakula kizuri na kupeleka watoto shule.

Katika hatua nyingine Mkuu huyo wa Mkoa ameagiza Maofisa Ugani na Kilimo kutoka Ofisini na kwenda kutoa elimu kwa wakulima ikiwemo wanaolima korosho juu ya kanuni za kilimo bora.

Amesema Maofisa hao wanatakiwa kutumia muda zaidi kutembelea wakulima mashambani ili wakulima waweze kuzalisha mazao mengi ambayo yatawawezesha kuinua uchumi wao na mkoa kwa ujumla.

Dkt.Sengati amesema Serikali imewasomesha na kuajiri ili waweze kutoa elimu ya kilimo bora kwa wakulima kwa ajili ya kuleta mapinduzi makubwa katika uzalishaji wa mazao mbalimbali yakiwemo ya chakula na biashara na hivyo hawapaswi kuwa Ofisini wakati wakulima wakikabiliwa na matatizo mbalimbali yanayowarusha nyuma katika uzalishaji.