October 7, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Rais Samia awatua ndoo kichwani wanawake Manienga

Na Mwandishi wetu,Timesmajira

Wanawake katika Kijiji cha Manienga Kata ya Mawindi wilaya ya Mbarali Mkoani Mbeya wameishukuru serikali chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwajengea visima kupitia Mradi wa Kuboresha Usimamizi wa Maliasili na Kukuza Utalii Kusini mwa Tanzania (REGROW) ambavyo vinawasaidia kupata huduma ya Maji safi na salama kwa sasa na kuondokana na adha waliyokuwa wanakutana nayo kabla ya kujengewa visima hivyo.

Wanawake hao wamesema kwa kipindi kirefu wameteseka kwa kuokosa huduma ya Maji safi na salama ambapo walilazimika kutumia maji ambayo pia mifugo walikuwa wakinywa kupitia mito na katika kipindi cha kiangazi walilazimika kuchimba Makorongo ili kuchota maji kwa ajili ya matumizi ya nyumbani.

“Kipindi cha nyuma ilikuwa shida kubwa, tulikuwa tunatumia maji binadamu na ng’ombe kwa wakati mmoja, katika msimu wa kiangazi mto Kyoga ulikuwa unakauka tulikuwa tunalazimika kuchimba Makorongo ndani ya Mto huo ili tuchote maji ambapo pia Wafugaji walikuwa wanaleta mifugo kunywesha Maji hayo hayo na mifugo hiyo unakuta inayachafua maji,”amesema Mwanamama Koga Mkazi wa kijiji cha Manienga

Amesema walikuwa wanakunywa maji yananuka mkojo wa ng’ombe na kuyafuata umbali mrefu hivyo wameahidi kuitunza miundombinu hiyo ya maji iliyojengwa na Bodi ya Maji Bondo la Mto Rufiji kwa usimamizi wa Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Mradi REGROW kwa fedha za Mkopo wa masharti nafuu kutoka Benki ya Dunia ili idumu na wasirudi kuteseka na adha ya Maji kama Kipindi Cha nyuma.

Aidha afisa Maji kidakio cha Mto Great Ruaha Abisai Chilunda kutoka Bodi ya Maji ya Bonde la Mto Rufiji amesema kupitia Mradi wa REGROW kiasi cha Shilingi Milioni 600 wameweza kujenga Ofisi 10 za Jumuiya za watumia Maji katika Wilaya za Mufindi, Makete, Mbarali na Wanging’ombe kwa lengo la kuboresha huduma ya upatikanaji Maji safi na salama kwa wakazi wa maneno hayo.