October 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Rais Magufuli amnunulia Askofu Shoo viatu

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online, Kilimanjaro

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.John Magufuli Oktoba 22, 2020 amemnunulia Askofu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) jozi moja ya viatu bora vya ngozi kwa ajili ya mkewe Mama Janeth Shoo.

PICHANI: Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiteta jambo na Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania Dkt. Fredrick Shoo mara baada ya kuzindua Kiwanda cha Bidhaa za Ngozi cha Kilimanjaro International leather Industries Co Ltd kilichojengwa kwenye eneo la Gereza Kuu la Karanga Moshi mkoani Kilimanjaro jana.

Dkt.Magufuli amefanya ununuzi huo baada ya kuzindua kiwanda cha bidhaa za ngozi cha Kilimanjaro (Kilimanjaro International Leather Industries Co. Ltd) kilichojengwa katika eneo la Gereza Kuu la Karanga Moshi mkoani Kilimanjaro kwa ubia wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (PSSSF) na Jeshi la Magereza Tanzania.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimkabidhi zawadi ya viatu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania Dkt. Fredrick Shoo kwa ajili ya mke wake mara baada ya kumnunulia katika Kiwanda cha Bidhaa za Ngozi cha Kilimanjaro International leather Industries Co Ltd kilichojengwa kwenye eneo la Gereza Kuu la Karanga Moshi mkoani Kilimanjaro jana mara baada ya kukizindua. Picha na Ikulu

Hatua hiyo ni ishara njema na ujumbe kwa Watanzania kwamba licha ya kupaswa kudumisha umoja na mshikamano bila kujali imani, itikadi za kisiasa pia wana nafasi kubwa ya kuhakikisha wananunua bidhaa za ndani ili kusaidia kuimarisha uchumi na kuharakisha maendeleo.

Mradi wa ujenzi wa kiwanda hicho umehusisha uboreshaji wa kiwanda cha zamani kilichojengwa na Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere mwaka 1978 kwa ajili ya kuzalisha viatu vya kijeshi ambapo kilikuwa kikizalisha jozi 150 kwa siku, na sasa kimeboreshwa na kuongeza uzalishaji hadi kufikia viatu 400 kwa siku.