September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Polisi, TIO waendesha mafunzo ya usuluhishi

Na David John,TimesMajira Online. Mwanza

JESHI la Polisi mkoa wa mwanza kwa kushirikiana na Ofisi ya Usuluhishi wa Migogoro ya Bima (TIO), imeendesha mafunzo ya usuluhishi ya migogoro bima huku Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Naibu Kamshina Muliro Jumanne akiwata Askari hao baada ya kupata mafunzo kwenda kutenda haki.

Kamanda Muliro amesema ni matumaini yake kwamba askari wake baada ya kupata mafunzo, yatakwenda kuwaongezea weledi katika shughuli zao hususan kwenye masuala yanayohusu bima dhidi ya jamii.

Muliro ameyasema hayo jaana jijini hapa wakati akifungua mafunzo hayo, ambayo yalikuwa chini ya Mkuu wa Kitengo cha Usalama Barabarani, RTO Joyce Kutechi kwa kushirikiana na TIO.

“Natambua kuwa hapa kuna askari kutoka wilaya zetu zote zilizopo mkoani Mwanza kwa maana Ukerewe,Ilemela, Nyamagana, Sengerema, Magu, Kwimba, hivyo ni matumaini yangu mtasikiliza kwa makini na mkitoka hapa mtakwenda kuwaelekeza wengine,” amesema Kamanda Muliro.

Amefafanua kuwa katika ofisi yake, kuna migogoro ya malalamiko mengi kuhusu mambo ya bima na kwa kupitia mafunzo hayo, matarajio yake ni kuona mabadiliko makubwa na kwenda kuzingatia weledi.