March 7, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Othman:Tanzania kujipatia medani ya kimataifa kuridhia mikataba sita ya ILO

Na Mwandishi wetu,Timesmajira

KAMISHNA wa Kazi na Uchumi Kamisheni ya kazi Wiazara ya Kazi na Uwekezaji Zanzibar, Rashid Khamis Othman amesema kuwa Tanzania itajipatia heshima kubwa katika medani ya kimataifa kama ikiridhia mikataba sita ya Shirika la kazi Duniani (ILO).

Kamishna Othuman amebainisha hayo jana  jijini Dar es Salaam wakati akifungua kikao cha siku mbili kilichoratibiwa na Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) kwa kushirikiana na ILO cha uhamasishaji na ujengaji uwezo wa Mikataba sita ya Shirika la Kazi Duniani,alitaja mikataba hiyo  ni pamoja  mkataba namba C102,C121,C122,C155,CI87  na C189.

Amesema mikataba hiyo ambayo inalenga kuimarisha haki za msingi za wafanyakazi, usalama na afya sehemu za kazi, pamoja na kuhakikisha mazingira salama ya ajira, imekuwa sehemu ya mazungumzo ya muda mrefu kidogo baina ya ILO na Serikali ya Tanzania. 

“Tanzania tayari tulisharidhia mikataba 37 ya ILO na kama tutakwenda kuridhia hii sita mengine basi tutatengeneza heshima nzuri na hasa ukizingatia kwamba mikataba hii kwa kiasi kikubwa tayari tunaitekeleza  ikiwemo hata ile ya msingi inayohusika na usalama na afya kazini,” amesema

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu Tucta, Rehema Ludanga amesema  mikataba hiyo inalengo la kulinda utu, heshima za wafanyakazi, kuimarisha maslahi yao, kuhakikisha haki zao za msingi zinalindwa, na kutoa mwongozo madhubuti wa kushughulikia majeraha au ajali zinazotokea sehemu za kazi.

“Endapo tutafanikiwa jambo hili ninyi mliopo hapa mtakuwa mmefanikiwa kwa faida ya watanzania wote, sina shaka nah atua ambayo tumefikia maana tulipoanza ni parefu safari iliyobakia ni fupi, tuendelee kumuomba Mungu aweze kutusaidia ili jambo hili lifanikiwe,” amesema Ludanga

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi wa Shirika la Kazi Duniani (ILO), Caroline Mugalla, Mratibu wa Mradi wa Kukuza Utambuzi na Kuboresha Mazingira ya Kazi kwa Wafanyakazi wa Nyumbani kama watoa huduma kutoka ILO ,Chiku Semfuko anesema kikao hicho kinaonyesha dhamira ya pamoja ya kuimarisha haki za wafanyakazi, ushindani wa biashara, na maendeleo ya ajira zenye staha nchini.

Ameeleza kuwa majadiliano yatakayofanyika kwa siku mbili  yatatusaidia kuona hatua zilizofikiwa, changamoto zilizopo, na mikakati ya kuharakisha mchakato wa kuridhia na kutekeleza mikataba hiyo sita ya ILO.

“Tunawashukuru TUCTA kwa uratibu, na tunathamini ushiriki wa serikali, waajiri, na vyama vya wafanyakazi. Ushirikiano wa kijamii ndio msingi wa kazi za ILO, tutaendelea kutoa msaada wa kitaalamu wakati wote wa safari hii,” amesema Semfuko

Aidha Isaya Thomas kutoka Chama cha Waajiri Tanzania (ATE) amesema wao  wapo katika kuelimisha waajiri ili wapate uelewa juu ya mikataba hiyo inayolenga kuhakikisha haki za mfanyakazi na waajiri hazipotezwi badala yake zinalindwa.