October 1, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

NHC Arusha yapongezwa kukusanya Bil 5.2 ndani ya miezi nane

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula amelipongeza Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) mkoa wa Arusha kwa kufanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi Bilioni 5.230,483,727.90 katika kipindi cha kuanzia Julai 2022 hadi Februari 28 mwaka huu.

Kiasi hicho cha pesa kilichokusanywa ni asilimia 68 ya malengo ya makusanywa yaliyowekwa na Shirika kwa mkoa huo katika mwaka wa fedha 2022/2023 ya kukusanya shilingi Bilioni 7.68.

Dkt Mabula alisema kiasi hicho cha fedha kilichokusanywa ni cha kupongezwa na kinaonyesha namna watumishi wa shirika hilo katika mkoa wa Arusha wanavyofuatilia makusanyo ya kodi za nyumba za Shirika la Nyumba la Taifa.

Kwa mujibu wa Dkt Mabula, utaratibu unaotumiwa na ofisi hiyo ya NHC mkoa wa Arusha kuwakumbusha wateja wake mapema kabla ya tarehe ya mwisho ya kulipa kodi ni mzuri na unawafanya wateja hao kulipa kodi kwa wakati.

‘’Utaratibu mnaotumia kuwakumbusha wateja wenu kulipa kodi mapema kabla ya mwezi unaofuata ni mzuri na unawajengea displine ya wateja kutokuwa na malimbikizo ya madeni hapa niwaombe muendelee kuwakumbusha wateja wenu na pale inapolazimika kumuondoa mteja aliyeshindwa kulipa kodi basi itumike njia ya kistaarabu kwa lengo la kutunza utu na heshima yake’’ alisema Dkt Mabula.

Meneja wa Shirika la Nyumba la Taifa mkoa wa Arusha Benit Masika alimuambia Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuwa, pamoja na ofisi yake kufanikiwa kukusanya kiasi hicho cha pesa ndani ya miezi nane lakini NHC mkoa wa Arusha inatarajia kuvuka malengo ya makusanyo kwa kwa kipindi kilichobaki cha miezi minne kutokana na utaratibu waliojiwekea wa  kuwafuatilia kwa karibu wateja wake ili walipe kodi kwa wakati.

‘’Mhe waziri kinachotusaidia sisi katika kukusanya mapato  ni ufuatiliaji wa karibu kwa wapangaji wetu na wale wanaoshindwa kutekeleza wajibu wao wa kulipa kodi kwa wakati basi tunawaandikia notisi ya kuvunja mkataba mapema tu mwanzo wa mwezi unaofuata na wengi hawapendi kuvunjiwa mkataba’’ alisema Masika.

Katika hatua nyingine Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula amekagua miundombinu wezeshi ya kuelekea katika mradi wa Shirika la Nyumba la Taifa wa Safari City uliopo eneo la Burka Mateves ndani ya jiji la Arusha.

Ukaguzi huo umelenga kuangalia changamoto za barabara kuelekea eneo la mradi ambapo hata hivyo changamoto hiyo imeanza kutatuliwa na Wakala wa Barabara vijijini na Mijini (TARURA) kwa kuanza ujenzi wa daraja linalounganisha barabara ya mzunguko ya Afrika Mashariki (Bypass).

Akiwa katika eneo la daraja hilo, Dkt Mabula mbali na kuipongeza TARURA kwa hatua walizozichukua za kujenga daraja hilo ametaka ujenzi wake kuharakishwa kabla ya kuanza mvua za masika,

‘’Kwanza niwapongeze TARURA kwa hatua walizozichukua za kuanza ujenzi lakini niwaombe waharakishe ujenzi kabla ya mvua kuanza maana mvua zikianza kazi itakuwa ngumu’’ alisema Dkt Mabula

Mradi wa Safari City wenye ukubwa wa eneo la ekari 587 una jumla ya viwanja 1913 kwa ajili ya uendelezaji wa nyumba za makazi, majengo ya biashara, huduma za jamii kama shule, vyuo, hospitali, sehemu za ibada, michezo na tayari viwanja 1,030 katika eneo hilo vimeuzwa huku viwanja 573 vikiwa sokoni.

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula akizungumza na watumishi wa Shirika la Nyumba la Taifa mkoa wa Arusha alipotembelea ofisi za shirika hilo tarehe 2 Machi 2023.
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula akimsikiliza Meneja wa Shirika la Nyumba la Taifa mkoa wa Arusha Benit Masika alipotembelea ofisi za shirika hilo tarehe 2 Machi 2023. Kushoto ni Mwanasheria wa NHC mkoa wa Arusha Neema Mapunda.
Sehemu ya watumishi wakimsikiliza Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula alipotembelea ofisi za Shirika la Nyumba la Taifa mkoa wa Arusha tarehe 2 Machi 2023.
 Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula akifafanua jambo mbele ya mhandisi wa TARURA wilaya ya Arusha Albert Kyando wakati alipokwenda kuangalia changamoto za miundombinu wezeshi kuelekea mradi wa Safari City uliopo Burka Mateves tarehe 2 Machi 2023.
Eneo la daraja linalounganisha barabara ya mzunguko ya Afrika Mashariki (Bypass).
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula akikagua changamoto za miundombinu wezeshi kuelekea mradi wa Safari City ulipo eneo la Burka Mateves Arusha tarehe 2 Machi 2023.