July 4, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Nchi 26 zatarajia kushiriki maonesho ya SABASABA

Na Mwandishi wetu, Timesmajira

IMEELEZWA kuwa nchi 26 zinatarajia kushiriki katika maonesho ya 48 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam ‘Sabasaba’ huku ongezeko hilo likitokana na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kukuza Diplomasia ya kiuchumi.

Akizungumza jijini Dar es Salaam leo, Kaimu Mkurugenzi wa Usimamizi wa Biashara, Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania(TANTRADE), Crispin Luanda alisema maonesho hayo yanatarajiwa kuanza Julai 28 mwaka huu Ijumaa ya wiki hii

Ametaja miongoni mwa baadhi ya nchi zitakazoshiriki ni pamoja na China, Korea Kusini, Singapoli, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Afrika ya Kusini, Msumbiji na Kenya.

Akitaja sababu ya kilichochangia nchi hizo kuongezeka kushiriki maonesho hayo tofauti na miaka ya nyuma ni Diplomasia ya kiuchumi ambayo Rais Dk. Samia amekuwa akizunguka katika nchi mbalimbali kuhamasisha masuala ya biashara na uwekezaji.

”Rais Dk. Samia amekuwa akisimamia 4R kwa maana ya maridhiano, kukaa pamoja, kuzungumza, kujadili masuala ya biashara na hali hiyo imekuwa ikiwavutia watu wengi zaidi.

“ Tunamatumaini mwaka huu washiriki katika nyanja mbalimbali wataongezeka kulinganisha na mwaka jana kutokana na hamasa na maboresho yanayofanyika.

Akizungumza kwa niaba ya Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Mairi Makori amesema kazi ya jeshi la polisi ni kulinda raia na mali zao na katika uwanja huo kamati ya usalama watahakikisha wanafanya nayo kazi bega kwa bega katika kulinda.

“Mpango kazi tiliojiwekea katika kuimarisha ulinzi ni kuwepo na kituo cha polisi kitakachofanya kazi kwa saa 24, hatutategemea kuona uhalifu ukitokea kwani milango yote ya kuingia na kutoka tumeweka ulinzi, kutakuwa na kikosi cha mbwa na farasi na doria kufanyika ndani na nje ya uwanja,” amesema.

Naye Mmoja wa washiriki wa maonesho hayo,Isabela Muro amesema wamejiandaa vizuri kushiriki maonesho hayo ambayo kwa mwaka huu yanaonekana kuwa mazuri zaidi kuliko miaka ya nyuma.

Amesema kwa kiasi kikubwa mwaka huu kwani Serikali imeweza kufanya maandalizi mazuri ambayo yanatia hamasa kwao katika ufanyaji wa biashara.

“Maonesho ya mwaka huu, serikali imejiandaa vizuri, maandalizi ni mazuri hivyo tumejiandaa vizuri kuwahudumia watanzania,” amsema.