October 8, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

NBAA yatangaza matokeo ya Mei 2024

Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu (​NBAA), CPA Pius A. Maneno

Na Iddy Lugendo, Timesmajira Online DSM

BODI ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA) imeidhinisha matokeo ya mitihani ya 99 ya bodi kwa watahiniwa waliofanya mitihani hiyo 6,960 ambapo kati ya hao watahiniwa 4,549 wamefaulu ikiwa ni sawa na asilimia 65.4 huku ufaulu ukishuka kwa asilimia 1 ukilinganisha na muhula uliyopita wa mwezi mei 2023.

Watahiniwa waliosajiliwa walikuwa 7,602 watahiniwa 642 sawa na asilimia 8.4 hawakuweza kufanya mitihani kwa sababu mbalimbali, hivyo idadi ya watahiniwa waliofanya mitihani hiyo ni 6,960 sawa na asilimia 91.6 kati ya watahiniwa waliofanya mitihani 3,610 sawa na asilimia 51.9 walikuwa wanawake na watahiniwa 3,350 sawa na asilimia 48.1 walikuwa ni wanaume.

Mkurugenzi Mtendaji wa NBAA CPA Pius Maneno amesema katika muhula kama huu wa mei 2023 idadi ya watahiniwa waliofaulu mitihani yao walikuwa 4,205 sawa na asilimia 66.4 ukilinganisha na muhula huu ambao ufaulu ni asilimia 65.4 kuna tofauti ya asilimia moja katika ufaulu.

“Bodi inawapongeza wale wote waliofuzu mitihani yao na kuwataka wale ambao hawajafuzu kutokata tamaa bali waongeze bidii zaidi katika masomo yao ili waweze kufanya vizuri katika mitihani ijayo ya bodi” amesema CPA Maneno

Hivyo, Bodi inawashauri wanafunzi kuendelea kutumia vyema vitabu vilivyotayarishwa na bodi katika kujiandaa kwa mitihani yao, pia wanashauriwa kusoma vitabu vingine vya ziada ili kuongeza ufahamu zaidi katika masomo hayo.