October 7, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

NARCO yatakiwa kuwapa eneo kiwanda cha Union Meat

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega ameilekeza Bodi ya Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO ) kuwapatia eneo Kiwanda cha Machinjio cha Union Meat ili walitumie kupokelea na kunenepeshea mifugo ili kiwanda kiwe na uhakika wa kupata mifugo bora kwa ajili ya kuchinja na kuuza ndani na nje ya nchi.

Waziri Ulega ametoa maelekezo hayo wakati alipotembelea Kiwanda hicho cha machinjio kilichopo wilayani Kibaha, mkoani Pwani Agosti 26, 2024.

“Nailekeza bodi ya NARCO kuhakikisha ndani ya mwezi mmoja wawe tayari wameshaanda mkataba na kufanya makabidhiano ya eneo hilo kutoka katika Ranchi ya Ruvu na kuwakabidhi Kiwanda hiki cha Union Meat haraka iwezekanavyo”, amesema

Aidha, amekitaka kiwanda hicho kuwa na mkakati mzuri wa kuvutia wafugaji na wafanyabiashara kwenda kupeleka mifugo yao kuuza katika kiwanda hicho kwani kwa kufanya hivyo itawasaidia wao kuwa na uhakika wa malighafi kiwandani hapo.

“Ni muhimu sana muweke bei nzuri, na malipo kwa wanaoleta mifugo yao yafanyike kwa wakati, na kuwe na uwazi wakati wa kupima uzito wa mifugo katika mzani, mkifanya hivyo mtaweza kuwavutia wafugaji na wafanyabiashara wengi kuleta mifugo yao hapo na kuwezesha kiwanda kuwa na uhakika wa malighafi ya kutosha”, alibainisha

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda cha Union Meat, Miriam Ng’wandu amesema Kiwanda hicho kitakapoanza kufanyakazi kitawanufaisha Watanzania zaidi ya 1000 kupata ajira.

Alibainisha kwa kusema kuwa wao wapo tayari kwa kuanza uzalishaji wakati wowote, isipokiwa wanaomba eneo kwa ajili ya kukusanyia wanyama kwa sababu kiwanda hicho kinahitaji wanyama wengi wa kuchinja.