June 11, 2025

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Msakuzi Marathon yaja na mbiondani ya hifadhi Msitu wa Pande

Na Mwandishi wetu,Timesmajira

UNAWEZA Ukasema hizi ni mbio za Marathon ya aina yake na hazijapata kutokea sehemu yoyote nchini.

Upekee wa Marathon hiyo unatokana na ukweli kwamba zinafanyika ndani ya Msitu wa Hifadhi wa Pande uliopo wilaya ya Ubungo, jijini Dar es Salaam huku washiriki wakiangalia uoto wa asili na kupishana na wanyama wanaovutia ndani hifadhi hiyo.

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Pindi Chana, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika mbio hizo za Marathoni zilizoandaliwa na taasisi ya Kukuza Michezo, Mzakuzi Sports Promotion (MSP), yenye makazi yake, Mbezi Msakuzi. Hifadhi ya Msitu wa Pande, inasimamiwa na Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori nchini (TAWA) ambao wamechangia na kurithia mbio hizo zitakazofanyika Julai 12 kama sehemu ya kuutangaza utalii wa Msitu wa Pande.

Akizungumza na Waandishi wa habari jana, Mratibu wa Mzakuzi Sports Promotion, Filbert Mosha amesema kuwa mbio hizo zitakuwa za kilomita 2/5, kilomita 10 na kilomita 21.“Hizi mbio ni za aina yake, hazijapata kutokea nchini.

Tofauti yake ni kwamba unakimbia ndani ya Msitu wa Hifadhi ya Taifa huku ukiangalia wanyama, unakimbia huku unapishana na swala, unakimbia huku unamwangalia twiga, Pundamilia na wanyama wengine wengi, unakosaje kwa mfano burubani kama hii,” amesema Mosha

Amesema mbali ya mgeni rasmi, Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Pindi Chana, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Challamila, Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Albert Msando na watakuwa wageni maarufu watakaonogesha mbio hizo.

Kwa mujibu wa Mosha, mbio hizo ni mtoko na fursa pekee za kuutangaza utalii, kufurahia uoto wa asili na mandhali tulivu ya Msitu wa Pande unaopambwa na vivutio vya wanyama.

Ili kujisajili katika mbio hizo, Mosha anasema kila mshiriki anapaswa kujisajili kwa ada ya sh 35,000.

Anasema ada hiyo itamwezesha kila mshiriki mbali ya kukimbia, kutapata pia nyama choma ya pori, vinywaji laani, burudani ya muziki kutoka kwa moja ya bendi maarufu nchini na surprise nyingine kibao.

Naye Mwenyekiti wa Msakuzi Sports Promotion, Dk. John Kisimbi, amesisitiza kuwa tayari Waziri Dk. Pindi Chana amethibitisha kushiriki na Mkuu wa Mkoa Challamila, naye amethibitisha kwamba siku hiyo atakuwepo kutangaza utalii wa Hifadhi ya Pande.

“Mkuu wa Mkoa Mheshimiwa Challamila juzi tulikuwa naye kwenye Msitu wa Pande kuangalia maandalizi. Kwanza amefurahi na amepongeza wazo la kufanya Marathon kwenye Msitu wa Pande ili kukuza utalii wa mkoa wa Dar es Salaam, pili ameahidi ofisi yake itatoa ushirikiano wa kutosha kufanikisha mbio hizo, kwahiyo tunaishuru sana Serikali kwa kutuunga mkono,” amesema Dk. Kisimbi.

Amesema zaidi ya watu 1000, wanatarajia kushiriki mbio hizo, hivyo aliwataka wananchi kutoka sehemu mbalimbali za mkoa wa Dar es Salaam nan je ya mkoa huo, kuja kushiriki ‘mtoko’ huo, kujionea maajabu ya Hifadhi ya Msitu wa Pande.

Ameipongeza TAWA kwa kuwaruhusu kuandaa mbio hizo ndani ya hifadhi ya Pande na amewashukuru kwa namna walivyojitoa kufanikisha marathon hiyo.ends