September 21, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mlele waanza kutekeleza agizo la Rais Samia

Na George Mwigulu,Timesmajiraonline,Mlele

AFISA Lishe wa Wilaya ya Mlele, Amina Ali
amesema kuwa Serikali imeendelea kutoa huduma ya chakula shuleni kwa asilimia 100 ili kuboresha hali ya lishe na kutokomeza udumavu.

Ali amesema hayo Septemba 10,2024 wakati akisoma taarifa mbele ya kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2024, Godfrey Mnzava ambapo amesema wilaya hiyo imeanza kutekeleza agizo la Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan aliyoyatoa kwa serikali ya Mkoa wa Katavi wakati akifunga wiki ya Jumuiya ya wazazi wa chama cha mapinduzi (CCM)Julai, 2024 akiwataka kudhibiti udumavu unaotokana na lishe duni.

“Shule 38 za msingi na sekondari tumefanikiwa kuhakikisha lishe bora inatolewa”amesema Afisa huyo akijivunia mafanikio ya kuanzisha kitengo maalumu cha kutoa matibabu ya utapiamulo mkali katika vituo vitatu vya afya pamoja na hosptali ya wilaya ya Mlele.

Aidha amesema wameanzisha klabu 38 za afya lishe huku wakiendelea kutoa elimu ya lishe katika vituo 16 vya kutolea huduma ya afya na jamii kupita maadhimisho ya lishe kwa watoto chini ya miaka mitano, watu wazima na vijana.

Ali ameeleza kuwa halmashauri ya wilaya ya Mlele ina watoto 11,093 walio na umri wa miaka mitano ambapo kwa mwaka 2023/24 watoto 74 wana utapiamulo mkali kati ya watoto 9724 waliofanyiwa tathimini ya hali ni sawa na asilimia 0.8 ya utapiamlo mkali.

Ameeleza kuwa Mkoa wa Katavi kwa mujibu wa wataalamu wa afya takwimu zinaonesha kuwa kwa mwaka 2015/16 hali ya udumavu mkali ulikuwa asilimia 38.2 ambapo kwa sasa imepungua kwa asilimiia 32.2 kwa mwaka 2022.

Naye kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa, 2024,Godfrey Mnvaza amewataka wataalamu wa afya kutoa elimu ya umuhimu wa lishe bora ili kuweza kutokomeza udumavu wa watoto.

Mnvaza amesema kuwa udumamvu unasababishwa na mtindo wa maisha ya watu usiozingatia uandaaji wa chakula wa uwiano sahihi wa virutubisho vya chakula unaozingatia makundi matano ya chakula.

“Twendeni tukaisaidie jamii yetu ibaadilike na kuacha tabia ya mtindo wa maisha ili iweze kuondokana na hali hatarishi ya udumavu.

“Kuna watu bado wanachangamoto ya lishe duni unaoathiliwa na mtindo wa tabia ya maisha wanakulaje, wanaandaje chakula na utaratibu gani wa kuagalia uwiano wa ulaji” Amesema.

Mkazi wa Kijiji cha Mgombe, Mariam Rashidi amesema kuwa wao walikuwa wanalisha watoto wao chakula bila kuzingatia lishe bora kwa sababu ya kutokujua namna bora ya uandaaji wa chakula utakao tokomeza udumavu.

Amesema kuwa kupitia elimu ambayo wanaendelea kupewa na wataalamu wa afya itawasaidia kuacha tabia ya kuandaa chakula kiholela.

Aidha Mwenge wa Uhuru wilayani humo umetembelea miradi sita yenye thamani ya Bil 1.7 ikiwa ni pamoja na mradi wa ujenzi wa barabara ya lami yenye urefu wa km 1.5 wa Mil 838.8, Mradi wa kikundi cha vijana cha muziki cha jitihada na maendeleo wenye thamani ya mil 10.

Mradi mwingine ni kuzindua ujenzi wa zahanati kijiji cha Songambele wenye thamani ya MIL 155.4, Kuzindua ujenzi wa shule ya sekondari Mlele wenye thamani ya Mil 650.8, Mradi wa uhifadhi wa mazingira (Kiwanda cha kuchakata asali Inyonga) wa Mil 50 na ujenzi wa vyumba viwili vya madarasa shule ya msingi Mgombe wenye thamani ya Mil 63.7.