September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mjane amwangukia Rais Magufuli kuomba apate haki zake

Na Martha Fatael,TimesMajira Online,Moshi

MJANE Fatuma Moses(80),mkazi wa Manispaa ya Moshi,amemwamgukia Rais John Magufuli,kumsaidia apate haki yake kwa madai ya kutaka kuporwa haki yake ya kuwa msimamizi wa miradhi ya mumewe, Ally Mose.

Fatuma Moses(80),mkazi wa Manispaa ya Moshi

Katika kilio hicho,Fatuma ambaye amedai kusumbuliwa na matatizo ya kiafya amesema amemuomba Rais Magufuli kuingilia kati ili apate haki hiyo na kufanikiwa kutumia akaunti ya mumewe aweze kwenda kutibiwa nchini India.

Kauli hiyo inafuatia,Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi, kukataa kuitupilia mbali maombi ya rufaa yaliyodaiwa kupelekwa mahakamani hapo nje ya muda, yakiwa na lengo la kupinga maamuzi ya Mahakama ya Mwanzo yaliyompa mjane huyo haki ya kusimamia mirathi ya mumewe.

Akitoa uamuzi mdogo mahakamani hapo,Hakimu Mkazi Mfawidhi, Naomi Mwerinde, aliueleza upande wa mlalamikiwa Fatuma Mose kupitia wakili wake,Hassan Ally kwamba mahakama imetupilia mbali pingamizi lake la kutaka rufaa ya mlalamikaji,Hamis Omary isisikilizwe.

Fatuma Moses(80),mkazi wa Manispaa ya Moshi, akisaidiwa na wasamaria wema kutoka nje ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi kusikiliza kesi ya mirathi ya mume wale marehemu Ali Mose

Amesema amebaini rufaa ilikusudiwa kukatwa ndani ya muda lakini malipo yalifanyika siku sita baadaye, na kwamba mara kesi hiyo itakapofika tena Oktoba 13,2020 pande zote mbili zitaeleza sababu za kulipia rufaa nje ya muda uliotajwa kisheria na sababu za kuweka pingamizi hilo.

Hakimu Mwerinde alisema alifuatilia mihuri iliyokuwa imegongwa katika nyaraka za rufaa lakini ineonekana yupo karani anatakiwa aje aeleze sababu za yeye kuchelewa kutoa Control namba ili mleta maombi afanye malipo ya ufunguzi wa rufaa yake.

Hata hivyo wakili wa mjibu maombi,Hassan Ally, amesema anakusudia kukata rufaa mahakama kuu kupinga maamuzi ya mahakama hiyo kusikiliza rufaa iliyoletwa nje ya muda.