Na Mwandishi wetu, Timesmajira
Waziri wa Afya, Jenista Mhagama amesema juhudi za Serikali kupitia Wizara ya Nishati kufikisha umeme hadi maeneo ya Vijijini zinapelekea wananchi kupika kwa kutumia nishati iliyo safi kupitia majiko yanayotumia umeme kidogo.
Mhagama ameyasema hayo jijini Dodoma wakati akihamasisha wananchi kuachana na matumizi ya nishati isiyo safi na kuanza kupika kisasa kwa kutumia Nishati Safi ya Kupikia.
“Kutokana na uwepo wa umeme katika Vijiji, sasa Mwanamke mahali popote Tanzania anaweza kupika kisasa kwa kutumia nishati safi badala ya kuni na mkaa ambazo si nishati safi.” Amesema Mhagama
Amesema faida za matumizi ya nishati safi ya kupikia zinakwenda hadi katika ngazi ya familia kwa namna mbalimbali ikiwemo kuimarisha afya za wana familia.
“Magonjwa yanapoondoka kwenye familia hata gharama za matibabu zinaondoka na kama hakuna gharama za matibabu ina maana nguvu inaelekezwa katika maendeleo ya familia.” Ameeleza Mhagama
Ametoa rai kwa jamii kuachana na matumizi ya nishati isiyo safi kutokana na uharibifu wa mazingira kupitia ukataji miti kwa ajili ya kuni na mkaa na hivyo kusababisha madhara mbalimbali ikiwemo mafuriko na mvua zisizotabirika.
More Stories
Serikali yathamini mchango wa viongozi wa Dini kwenye maendeleo
Waziri Jafo awaasa wajumbe Bodi ya FCC kuwa waadilifu, waaminifu
Rais Samia: Hatua mpya katika maboresho ya mfumo wa kikodi Tanzania