October 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Magufuli aagiza anayetaka kuwekeza apewe vibali ndani ya siku 14

Na Waandishi Wetu, TimesMajira Online

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Magufuli ameamua kulihamisha suala la uwekezaji ikiwemo Kituo Cha Uwekezaji Tanzania (TIC) kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu kwenda Ofisi ya Rais ili aweze kupambana vizuri na wanaokwamisha wawekezaji.

Dkt. Magufuli ametoa agizo hilo leo jijini Dodoma wakati wa ufunguzi Rasmi wa Bunge la 12 Mkutano wa Kwanza kikao cha Nne wakati akilihutubia bunge.

Pia Rais Magufuli amesisitiza kuwa mtu mwenye mtaji anayehitaji kuwekeza hapa nchini apate vibali ndani ya siku 14 ili uwekezaji huo kusaidia taifa ili kuendelea kimaendeleo.

“Miaka mitano iliyopita tuliwachukulia hatua za kinidhamu watumishi 32,555 na kuiwezesha nchi yetu kushika nafasi ya kwanza kati ya nchi 35 za Afrika kwa kupambana na rushwa kwa kifupi niseme utumbuaji unaendelea”, ameeleza Rais Magufuli

Rais Magufuli amesema kuwa atashirikiana na rais wa Zanzibar Dkt. Hussein Mwinyi kulinda Amani, hawatokuwa na utani hata kidogo na mtu atakaye taka kuvuruga Amani na kuingilia uhuru wa Tanzania.

“Namuhaidi rais mwinyi ntampa ushirikiano wa kutosha katika kukamilisha aliyoyaahidi ili kutimiza adhima ya watanzania walio tuamini”, amesisitiza Rais Magufuli.

Lakini pia Rais Magufuli ameeleza kuwa Sekta ya utalii imeajiri watu takribani milioni nne kwenye miaka mitano iliyopita , sekta hiyo ilikuwa ikitoa mchango mkubwa ambao ulikuwa unaridhisha ambapo idadi ya watalii waliotembelea nchini iliongezeka pamoja na mapato pia.

“Naipongeza hifadhi yetu ya taifa ya Serengeti kwa kuchaguliwa kuwa hifadhi bora barani afrika mwaka huu”, amepongeza Rais Magufuli.

Rais Magufuli amesema kuwa miaka mitano ya ya uongozi  wake wa awamu ya pili watanunua meli nane za uvuvi ambapo meli nne zitakuwa Zanzibar nan ne Tanzania Bara ambapo zitafanya kazi kwenye bahari kuu.

Pia Rais Magufuli ameongeza kuwa serikali yake imepanga kupunguza foleni barabarani , itapanua viwanja vya ndege 11, kuboresha upatikanaji wa huduma za umeme , itafikisha umeme kwenye vijiji vyote vilivyobaki, na upande wa afya itahakikisha watanzania  wote wanakuwa na bima ya afya na kuongeza hospitali.

Hata hivyo Rais Magufuli amesema kuwa Katika miaka mitano ijayo amepanga kuimarisha usafiri wa reli ya kati na TAZARA, kukamilisha ujenzi wa reli ya kisasa kutoka Daer es salaam , Morogoro, hadi Dodoma.