September 23, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kishindo cha Rais Samia ni neema Rukwa

•Aridhia kuanzia msimu ujao wa Kilimo kuwe na ruzuku ya bei ya mbegu za mahindi.

•Aridhia Serikali kununua mahindi ya wakulima kwa shilingi 700/Kg

•Seminari ya Kahengesa yapata barabara ya lami ikiwa ni heshima kwa mwadhama Protase Rugambwa na viongozi wengine waliowahi kupita katika seminari hiyo maarufu.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan amehitimisha kwa kishindo ziara yake ndani ya Mkoa wa Rukwa kwa kuzindua, kuweka mawe ya msingi pamoja kukagua miradi ya mabilioni ya shilingi itakayonufaisha mamilioni ya wananchi wa mkoa wa Rukwa na mikoa jirani kiuchumi na kijamii pamoja na kuridhia kuanzia msimu ujao wa kilimo kuweka ruzuku katika mbegu za mahindi na mbolea.

Katika ziara ya Rais Samia siku ya leo iliangazia kwenye sekta ya Afya, Elimu, Kilimo na Miundombinu kwa kufanya upanuzi wa Hospital za wilaya za Sumbawanga Bilioni 13.7, Ujenzi wa vituo vya Afya 21 na zahanati 30 kwa gharama ya bilioni 9.4, Elimu ya ngazi chini shule mpya za msingi 9, madarasa ya awali 26, madarasa ya shule za msingi 150, matundu ya vyoo 251, nyumba za walimu 2 na ukarabati wa shule kongwe 1.

kwa upande Elimu ya Ngazi ya juu Chuo cha Veta Paramawe milioni 348, chuo cha Veta Kalambo Milioni 324, Chuo cha Maendeleo ya wananchi cha Chala bilioni 14, Chuo cha walimu Sumbawanga Bilioni 4.27, Upanuzi wa chuo cha Maafisa Tabibu Sumbawanga ikiwemo miundombinu ya barabara na miundombinu ya kilimo na kuhifadhi chakula.

Katika ziara ya leo Rais Samia amefungua utanuzi wa Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Tawi la Rukwa ambacho kimegharimu kiasi cha shilingi Bilioni 14.68, aidha amefika hadi kijiji cha Mtindilo Laela na kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa shule ya sekondari ya Wasichana ya Mkoa wa Rukwa.