October 7, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kikwete afunguka, asema Rais Samia ‘amemfunika’

Na Omary Mngindo,Timesmajiraonline, Bagamoyo

RAIS Mstaafu wa Serikali ya Awamu ya Nne, Dkt. Jakaya Kikwete, amempongeza Rais Dkt. Samia Suluhu, kwa namna anavyopeleka fedha katika halmashauri, zinazokwenda kutekeleza shughuli mbalimbali za maendeleo, ambapo miradi mingi inatekelezwa katika uongozi wake

Kikwete ametoa pongezi hizo katika Mkutano Mkuu wa Jimbo la Bagamoyo, ulioandaliwa na Mbunge, Muharami Mkenge, ambapo alisema aliposikia Chalinze imekuwa ya kwanza alifarijika sana.

“Nilipokuwa Rais nilijiona bingwa wa kupeleka fedha nyingi katika halmashauri zikilenga maendeleo, ukiachilia watangulizi wangu katika uongozi mimi nilipeleka fedha nyingi, lakini Rais Samia amenifunika,” amesema Dkt. Kikwete.

Kikwete pia alipongeza Halmashauri ya Chalinze kwa kuwa ya kwanza katika ukusanyaji wa mapato.

Ameongeza kuwa katika kumi bora za ukusanyaji wa mapato, Mkoa wa Pwani una Wilaya na Halmashauri tatu ambazo mbali ya Chalinze nyingine ni Mkuranga iliyoshika nafasi ya nne huku Bagamoyo ikikamata ya nane.

“Nitumie nafasi hii kuipongeza Halmashauri ya Chalinze kwa kushika nafasi ya kwanza kitaifa kwa ukusanyaji wa mapato kupitia vyanzo vyake vya ndani, hii inaonesha ni namna gani viongozi wake wanavyotekeleza majukumu yao kwa uhakika nawapongeza sana,” amesema Dkt. Kikwete.

Ameongeza kwamba; “Nizipongeze Mkuranga kwa kushika nafasi ya nne na Bagamoyo kuwa ya nane hivyo kuwa kwenye kumi bora, niwatie nguvu muendelee kuongeza nguvu katika kukusanya fedha zitazosaidia kupunguza kama si kumaliza changamoto katika maeneo yenu,” alisema.

Katika hatua nyingine Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limeanza kuhudumia wateja wake kidijitali kupitia mfumo wake wa NIKONECT ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Rais Samia Suluhu Hassan la kutaka mashirika ya umma yajikite katika matumizi ya mifumo ya kidijitali.

Hayo yamesemwa na Afisa Huduma kwa Wateja TANESCO, Fatuma Mohamed, wakati akizungumza na waandishi wa habari katika maonesho ya wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea jijijini Dodoma.

Amesema mfumo huo wa NIKONECT unatoa huduma kuanzia maunganisho ya umeme, huku akisema wamepanua wigo katika matumizi ya TEHAMA kwa upande wa kutoa taarifa kwa jamii.

“Kupitia mfumo wetu wa kidijitali wa NIKONECT , mteja sio lazima afike ofisini ili kupata huduma ya kuunganishiwa umeme, isipokuwa mahali popote mteja ,awe na simu au hata simu ya kitochi , anaweza kufanya maombi ya kuunganishiwa umeme na akapata huduma hiyo.”alisema Fatuma

Aidha amesema katika utoaji wa taarifa kwa kutumia TEHAMA, wigo umepanuka zaidi ambapo kwa kutumia mfumo wa JISOT mteja anaweza akatoa taarifa kwa njia ya simu yake ya mkononi.