September 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kata tano Ilala mbioni kuondokana na hadha ya maji

Na Agnes Alcardo,TimesmajiraOnline,Dar

MKUU wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, amewahakikishia wakazi wa Gongo la Mboto, kuwa ndani ya hii miezi mitatu wataondokana na hadha ya maji ambayo wamekuwa nayo kwa kipindi cha muda mrefu, ambayo sasa yataenda kuingia kwenye mradi wa maji wa tanki la Bangulo hadi kwa wananchi lenye ujazo wa Lita Mil moja na ukiwa na thamani ya Bil 36.

Akijibu miongoni mwa kero zilizowasilishwa na wakazi kutoka Kata za Gongo la Mboto, Pugu station, Pugu, Majohe na Ukonga, kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika leo kwenye Viwanja vya Kampala, Gongo la Mboto Jijini Dar es Salaam, ikiwa ni muendelezo wa ziara yake katika Wilaya ya Ilala.

Mpogolo amesema anatambua kero hiyo ni ya muda mrefu kwa wananchi wa ukanda huo, hivyo Serikali iliamua kuanzisha mradi wa ujenzi wa tangi kubwa la maji lililogharimu kiasi hicho kikubwa cha fedha.

“Kata ya Gongo la Mboto Pugu, Pugu Stesheni,Majohe, kivule kuelebe kwenda Kitunda , Buyuni, kata zote hizo zilikuwa na chngamoto ya maji Mheshimiwa Rais ametujengea tenki la maji karibu yenu tenki la lita Mil moja kwa thamani zaidi ya Sh Bil 36.7,” amesema Mpogolo.

Pia ameongeza kuwa, utekelezaji wa mradi huo umefika asilimia 64 hadi sasa na unatarajiwa kukamilika na maji kuanza kuingia katika mradi huo ili kuanza kusambazwa kwa wananchi wa maeneo hayo baada ya kipindi cha miezi mitatu.

Sambamba na hilo amesema kuwa katika suala la urasimishaji lipo katika hatua za mwisho na hadi sasa kuna hati zaidi ya 10,000 ambazo zipo tayari kwa ajili ya kufanyiwa utaratibu ili wananchi waweze kupewa hati hizo.