March 21, 2025

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kamati ya kudumu ya Bunge yapongeza ujenzi wa jengo la Wizara ya Nishati Mtumba

Na Mwandishi wetu, Timesmajira

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imekagua ujenzi wa jengo la Wizara ya Nishati katika mji wa Serikali Mtumba na kuipongeza Wizara kwa hatua ya ujenzi iliyofikiwa kwa asilimia 94.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo, David Mathayo amesema hayo tarehe 20 Machi 2025, wakati wa ziara ya kukagua ujenzi wa jengo hilo katika Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma iliyohusisha Menejimenti ya Wizara na baadhi ya watumishi.

“Tumepita kila mahali katika jengo hilo kazi nzuri na kubwa imefanyika na mandhari ya ndani na ya nje zote zinavutia sana, nawapongeza sana Wizara ya Nishati kwa kazi hii, zaidi kamati inampongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuhakikisha kuwa fedha zinapatikana za kutekeleza ujenzi wa majengo mengi na mazuri ya serikali,”amesema Mathayo


Amepongeza Viongozi Wakuu na Menejimenti ya Wizara ya Nishati kwa kusimamia vyema ujenzi huo na kuhakikisha fedha za mkandarasi zinalipwa kwa wakati wakati wote.

Aidha,amewasisitiza kukamilisha kazi ndogo zilizosalia ili watumishi waweze kuhamia katika jengo hilo mapema.

Kwa upande wake, Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Dkt. Khatibu Kazungu, amesema kuwa watumishi wa Wizara ya Nishati wanatarajia kuhamia katika jengo hilo kabla ya mwezi Mei 2025 kwa kuwa kazi kubwa tayari imeshafanyika.

Dkt. Kazungu amesema watumishi wote wakihamia katika jengo kutawazesha watumishi hao kukaa sehemu moja na kufanya kazi zao kwa ufanisi tofauti na ilivyo sasa ambapo watumishi wamegawanyika katika sehemu mbili ambazo ni Kikuyu na Mtumba.