October 2, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Dkt.Mpango afanya mazungumzo na Mkurugenzi Msaidizi wa Green Climate Fund

Na Mwandishi wetu, timesmajira

Makamu wa Rais Dkt. Philip Mpango amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Msaidizi – Uwezeshaji Sekta Binafsi wa Green Climate Fund, Soji Omisore, ambapo mazungumzo hayo yalifanyika Doha nchini Qatar.

Katika mazungumzo hayo Makamu wa Rais ametaja athari zinazoikabili Tanzania kutokana na mabadiliko ya tabianchi kama vile ukame, mafuriko, ongezeko la kina cha bahari ambazo zinapelekea changamoto katika sekta ya kilimo.

Makamu wa Rais amesema Tanzania imeendelea kufanya jitihada mbalimbali katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi ambayo inahusisha utengenezaji wa sera kama vile sera ya taifa ya mazingira, mkakati wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, kuandaa mpango kabambe wa mazingira pamoja na usafi na uhifadhi wa mazingira kupitia upandaji miti kila mkoa.

Makamu wa Rais ametaja jitihada zingine ambazo ni kuhamasisha matumizi ya nishati mbadala, kuwekeza katika uhifadhi wa misitu, kuvutia tekenolojia rafiki za mazingira pamoja na mchango wa taifa katika kupunguza gesi joto wa mwaka 2021.

Makamu wa Rais amesema Tanzania bado inahitaji kuungwa mkono katika kukabiliana na athari za mbadiliko ya tabia nchi kifedha, kiteknolojia pamoja na kuwajengea uwezo wataalamu katika kuandaa maandiko ya miradi yenye uwezo wa kupata ufadhili.

Pia ametoa wito kwa taasisi ya Green Climate Fund kuiunga mkono Tanzania katika utoaji elimu ya biashara ya kaboni na njia nyinginezo za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Kwa upande wake Mkurugenzi Msaidizi – Uwezeshaji Sekta Binafsi wa Green Climate Fund,Soji Omisore amesema taasisi ipo tayari kuendelea kushirikiana na Tanzania katika miradi ya uhifadhi wa mazingira.

Amesema taasisiya Green Climate Fund itajielekeza pia katika kuwajengea uwezo wa wataalamu wa Tanzania.

Green Climate Fund inafadhili miradi mbalimbali ya mazingira na mabadiliko ya tabianchi nchini Tanzania ikiwemo mradi wa Tanzania Agriculture Climate Adaptation Technology Deployment Programme (TACATDP) unaolenga kusaidia sekta ya kilimo katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Mazungumzo hayo yamehudhuriwa na Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Mwigulu Nchemba, Waziri wa Fedha na Mipango wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Dkt. Saada Mkuya,Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mbarouk N. Mbarouk pamoja na Naibu Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania Umoja wa Mataifa (New York) Balozi Dkt. Suleiman Haji Suleiman.Imetolewa na Ofisi ya Makamu wa RaisMachi 06,2023Doha Qatar