September 30, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Chama cha Ushirika chaisadia shule saruji

Na Julius Konala,TimesMajira Online. Ruvuma

CHAMA Kikuu cha Ushirika cha Wakulima wa Tumbaku Songea na Namtumbo (SONAMCU) mkoani hapa, kimechangia mifuko 35 ya saruji yenye thamani ya sh. 450,000 na fedha taslimu sh. 300,000 kwa ajili ya kutatua changamoto ya upungufu wa matundu ya vyoo, iliyokuwa ikiikabili Shule ya Msingi Msamala mjini Songea kwa muda mrefu.

Mchango huo umetolewa jana na Meneja Mkuu wa chama hicho, Juma Mwanga katika mahafali ya 38 ya Shule ya Msingi Msamala 2020 yaliyofanyika kwenye viwanja vya shule hiyo na kuhudhuriwa na wadau mbalimbali wa elimu, wakiwemo walimu wa shule jirani, wazazi na Waratibu Elimu Kata.

Mwanga amesema chama hicho, kimeamua kutoa mchango huo baada ya kuguswa na changamoto iliyokuwa ikiwakabili wanafunzi wa shule hiyo kwa muda mrefu, ili waweze kuepukana na magonjwa ya mlipuko.

“Ndugu Mwalimu Mkuu, nachukua nafasi hii kusema kwamba kutokana na shule hii kukabiliwa na changamoto ya upungufu wa matundu ya vyoo kwa muda mrefu, naahidi kuchangia tena pale chama kitakapokuwa na uwezo wa kupata fedha na kwamba nawaomba wadau wengine, wazazi na wananchi kuona umuhimu wa kuunganisha nguvu katika kuiunga mkono serikali kwenye uchangiaji, ili tuweze kutatua tatizo hilo,” amesema Mwanga.