September 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

CCM yatoa maagizo kwa serikali kuhakikisha pembejeo za Kilimo zinapatikana

Na Penina Malundo, Timesmajira

CHAMA cha Mapinduzi CCM kimetoa maelezo kwa serikali kuhakikisha pembejeo za kilimo zinapatikana kwa bei nafuu na kwa wakati,ili wananchi waendelee kulima kilimo cha tija.

Pia kimeitaka Serikali kuendelea kutekeleza wajibu wake wa kuhakikisha inatafuta masoko ya uhakika ili wakulima waweze kunufaika na kilimo chao.

Akizungumza hayo jana, Katibu Mkuu wa Chama hicho,Balozi Dkt,Emmanuel Nchimbi wakati akizungumza na wanachama wa chama hicho na wananchi katika uwanja wa sabasaba mkoani Mtwara,amesema kwa miaka michacheWanamtwara wamepiga hatua katika kilimo ambapo kuna kila dalili zinazoonyesha habari za umaskini zitabaki hadithi katika mkoa wa mtwara.

“Naiagiza serikali ihakikishe pembejeo za kilimo zinapatikana kwa wakati na kwa bei nafuu. Mikoa ya Kusini malalamiko ni mengi kuhusu jambo hilo. Hata masoko yapatikane”amesema

Dk. Nchimbi amesema serikali imetenga Sh.bilioni 150 kwa ajili ya upanuzi wa Bandari ya Mtwara.

Amesema tangu serikali iwekeze nguvu katika uendelezaji wa bandari hiyo matokeo chanya yameanza kuonekana ikiwemo ongezeko la mapato ya Sh.bilioni 25.

”Maelfu ya tani yanasafirishwa na kuletwa mkoani mtwara kupitia bandari hiyo,sasa hivi utegemezi wa bandari ya Dar es Salaam umepungua kwa kiasi kikubwa kutokana na uboreshwaji wa bandari hii ya Mtwara,”anasema na kuongeza

”Natoa wito kwa Serikali kuendelea kuimarisha bandari hii ambayo ni mkombozi wa mikoa ya kusini hii iwe tegemeo katika mikoa yetu na kuendelea kupunguza msongamano katika bandari ya Dar es Salaam na kufanya bidhaa zitoke kwa wakati na kuwafikia walengwa,”amesema.

Kuhusu Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, Dk. Nchimbi amewataka wanachama wa CCM kuhakikisha wanachagua wagombea wanaojua uongozi, waadilifu, wasiokuwa na chuki, visasi.

Pia, amewataka Watanzania kuendelea kudumisha amani, umoja na mshikamano, akisema kati ya nchi tatu Afrika zenye amani Tanzania ni mojawapo.