Fresha Kinasa,TimesMajiraOnline,Mara
KATIBU wa Siasa,Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Mara Simon Rubugu amesema kuwa, Chama hicho kimepokea kadi za wanachama wa Mkoa huo waliosajiliwa kwa mfumo wa Kielektroniki zipatazo 645,000, ambapo kinatarajia kuanza zoezi la ugawaji wa kadi hizo Machi 29, 2025, Mkoani humo.
Rubugu ameyasema hayo leo Machi 27, 2025, wakati akizungumza na Majira Online Makao makuu ya chama hicho Mjini Musoma na kusema kuwa,kadi hizo zimebooreshwa kisasa huku akitoa msisitizo kwa Wanachama wa CCM ambao bado hawajasaliliwa kujisajili kwani zoezi hilo ni endelevu.
Amesema,idadi ya kadi hizo ni zaidi ya asilimia 51 ya makisio ya Wapiga kura na zitasaidia kuwatambua wanachama wa Chama cha mapinduzi kuanzia ngazi ya matawi, Kata, Wilaya hadi Mkoa kabla ya kuingia katika uchaguzi unaotarajia kufanyika mwaka huu.
“Kadi hizi zitakuwa na faida kwa wanachama ikiwemo kuwatambua wanachama wote kwenye mfumo, urahisi wa kufanya nao mawasiliano, Mwanachama kuitumia kadi katika matumizi ya miamala, naomba wanachama wakati wanakwenda kuchukua kadi zao waende na Vitambulisho vyao vya NIDA au Kadi ya Mpiga kura kwa ajili ya kuingizwa kwenye mfumo.”amesema na kuongeza kuwa
“Tunashukuru sana juhudi thabiti zilizofanywa na Mwenyekiti wetu Taifa Ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhakikisha wanachama wanakuwa kwenye mfumo, haya ni mageuzi makubwa na mazuri sana kwa chama chetu .” amesema Rubugu.
Pia, amepongeza miradi ya maendeleo iliyofanywa na Serikali ya Chama Cha mapinduzi chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ikiwemo ujenzi wa miradi ya Kimkakati kama uwanja wa Ndege wa Musoma, Daraja la Magufuli Mwanza, Bwawa la Mwalimu Julius Nyerere, miradi mbalimbali ya elimu, afya, barabara, maji ambayo amesema itakipa ushindi wa kishindo Chama hicho kwenye uchaguzi Mkuu mwaka huu.
“Miradi ambayo imefanywa na Serikali uhakika ni kwamba chama kitashinda kwa ushindi mkubwa sana, hii ndio reforms ya maendeleo, miradi inaonekana kwa macho. Mkoa wa Mara tunao uwanja wa Ndege ambao utafungua fursa ya uchumi.Tunao mradi mkubwa wa maji wa Mugango-Kiabakari- Butiama huu umesaidia Wananchi wengi na mradi mwingine wa Maji upo wa Rorya unakwenda mpaka Tarime wa Bil. 134, Wananchi wamekoshwa na miradi hii.”amesema.
Aidha, amewataka wanachama wa Chama hicho Mkoa wa Mara kuendelea kushikamana, kupendana na kuachana na makundi madogo madogo. Na pia, waendelee kuyasema kwa Wananchi mema na maendeleo yote ambayo serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan inayafanya maeneo mbalimbali hapa nchini
More Stories
EWURA kinara uhusiano mwema na vyombo vya habari nchini
TANESCO yaibuka kinara tuzo za ubora za Mawasiliano na Uhusiano kwa umma 2024
Taasisi za uhifadhi zatakiwa kulinda maeneo ya hifadhi kwa teknolojia