October 8, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

BRELA yatoa wito wananchi kutumia fursa za maonesho kusajili  biashara zao

Na Zena Mohamed,Timesmajiraonline,Dodoma

WAKALA wa usajili wa biashara na leseni(BRELA) umetoa wito kwa wamiliki wa biashara kutumia fursa kunapokuwepo na maonesho ya watoa huduma hizo kusajili bidhaa zao na kupata elimu zaidi kwani watasajiliwa papo hapo.

Hayo yamesememwa jijini hapa leo Juni 20,2024 na Kaimu Meneja Rasilimali na Utawala BRELA,Migisha Kahangwa wakati akizungumza na Waandishi wa Habari katika Maonyesho ya Wiki ya maadhimisho ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park yanayokwenda na kaulimbiu ya “Kuwekeza kwa utumishi wa umma ulijikita kwa umma wa Afrika Karne ya 21 iliyojumuishi na inayostawi,ni safari ya mafunzo na mabadiliko ya kiteknolojia”.

Amesema kuwa kunafaida nyingi kwenye kusajili biashara yako au kampuni yako ambapo alitaja faida moja wapo kuwa hata wawekezaji wa nje ya nchi wakitaka kuja kuwekeza nchini wakati mwingine wanaangalia urahisi ulipo ambapo hukimbilia kuwekeza kwenye kampuni au biashara ambayo tayari imeshasajiliwa.

“Kila mwananchi ana haki ya kutoa huduma kwa maana ya kufanya biashara lakini ili kuwa na uhakika ni muhimu kujisajili ili biashara yako itambulike na iwe halali,”amesema.

“Napenda kutoa wito kwa wananchi  wote ambao wamekuwa wakijihusisha na kutoa huduma kwa wananchi kuhakikisha wanajisajili BRELA ili wapate faida na za ziada lakini wajitokeze kwa wingi katika maonesho kama haya kwani wanapata elimu pamoja na kusajiliwa hapa hapa,”amesema Kuhangwa.

Kwa upande Wake Afisa Usajili wa BRELA ,Gabriel Gilangay amesema kama BRELA wamekuwa wa Kitoa elimu kwa wanachi kuhusu huduma wanazozitoa huku akiwashauri Wananchi kujaza fomu namba 128 kwaajili ya kutoa taarifa kuhusu  usajili wao kama unafanya kazi au la.

Gilangay amefafanua kuwa endapo mtu hata jaza fomu hiyo wao hawatajua  kama  biashara aliyoisajili inafanyika au  la na  mwisho  wa siku wanaweza kuwafuta au kuwaondoa kwenye mfumo.