September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Afisa Maendeleo ya Jamii Bodi ya Maji Bonde la Kati, Halima Faraji, akitoa mafunzo kwa Wawakilishi wa Jumuiya ya Watumia Maji, Viongozi wa vijiji na kata wa Bwawa la Numbu ambao wapo katika mafunzo ya kuhifadhi vyanzo vya maji mkoani Shinyanga jana. Picha na Dotto Mwaibale

Bodi ya Maji Bonde yatoa mafunzo kuhifadhi vyanzo vya maji

Na Dotto Mwaibale, TimesMajira Online,Shinyanga

WAWAKILISHI wa Jumuiya ya Watumia Maji wa Bwawa la Numbu pamoja na viongozi wa vijiji na kata ambao wapo katika mafunzo ya kuhifadhi vyanzo vya maji mkoani Shinyanga wametakiwa kuzingatia kile wanachofundishwa ili wakawe mabalozi kwenye maeneo wanayotoka.

Afisa Maendeleo ya Jamii Bodi ya Maji Bonde la Kati, Halima Faraji, akitoa mafunzo kwa Wawakilishi wa Jumuiya ya Watumia Maji, Viongozi wa vijiji na kata wa Bwawa la Numbu ambao wapo katika mafunzo ya kuhifadhi vyanzo vya maji mkoani Shinyanga jana. Picha na Dotto Mwaibale

Ombi hilo limetolewa na Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii Manispaa ya Shinyanga, John Tesha kwa niaba ya mkurugenzi wa Manispaa hiyo wakati akifungua mafunzo hayo yalioandaliwa na Bodi ya Maji Bonde la Kati na kufanyika eneo la Songwa nje kidogo ya mji wa Shinyanga.

“Ninyi ndio mtakao kuwa mabalozi wa kwenda kutoa elimu kwenye maeneo yenu ya kulinda vyanzo vya maji nawaombeni mzingatie mafunzo haya ambayo ni ya muhimu sana,” amesema Tesha.

Akizungumzia mafunzo hayo Afisa Maendeleo Mwandamizi wa Bodi ya Maji Bonde la Kati,Nelea Bundara amesema kabla ya mafunzo hayo walifanya mikutano ya hadhara ya uhamasishaji juu ya utunzaji wa maji katika vijiji nane.

“Lengo la kuwakutanisha wadau hawa ni kwa sababu ya vijiji vinavyo zunguka vyanzo vya maji hususani Bwawa la Numbu na Songwa kuwa kumekuwa na uharibifu mkubwa wa mifugo kuharibu vyanzo vya maji, huku shughuli za kilimo zikifanyika mpaka ndani ya mabwawa haya ambayo yapo hatarini kutoweka kutokana na shughuli za kibinadamu” amesema Bundara.

Amesema kwa kuwa wao kazi yao kubwa ni kusimamia rasilimali za maji ili ziwe endelevu kwa vizazi vilivyopo na vijavyo wameona ni muhimu kuwepo na jumuiya ya watumia maji hususani Bwawa la Numbu ambalo wataanza nalo na kufuatia la Songwa na baadhi ya mabwawa mengine na kuhakikisha yanadumu na wanayatumia kwa mujibu wa sheria.

Bundara amesema sheria inaelekeza kwamba mtumiaji wa maji ndiye mtunzaji namba moja wa maji kwa sababu ni mnufaika na yupo maeneo ya vyanzo vya maji.

Alisema wametembea kwenye vijiji hivyo na kufanya mikutano na kupata wawakilishi watatu kutoka katika kila kijiji wakiwakilisha kundi la wafugaji, wakulima na matumizi ya nyumbani na kuwa sasa wapo darasani kuwafundisha ili waweze kujua umuhimu kwanza wa sheria na sera inasemaje na majukumu yao ya kusimamia rasilimali ya maji yapoje kisheria.

Amesema mafunzo hayo wamewashirikisha viongozi wa vijiji kwa sababu wao ni walinzi wa amani, wasimamizi wa kuu ngazi za vijiji hivyo jumuiya haiwezi kufanya kazi peke yake lazima washirikiane na vijiji.

“Viongozi wa vijiji na wawakilishi wa vijiji tumekaa darasani tukiamini tutakuwa na uelewa wa pamoja tukianzia kwa viongozi na wanajumuiya wenyewe wanaozunguka mabwawa hayo” amesema Bundara.

Aidha Bundara amesema katika mafunzo hayo wamewashirikisha wadau wengi kama Williamson Diamonds Limited wanao miliki Mgodi wa Almasi wa Mwadui na Bwawa la Numbu, Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu, Manispaa ya Shinyanga na Mwakilishi kutoka Ofisi ya Meneja wa Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) Wilaya ya Kishapu lengo likiwa kwa pamoja kama timu waweze kuunda kitu cha usimamiaji rasilimali za maji.

Amesema baada ya hapo wajumbe watakuwa na katiba na mpango kazi lakini pia rasimu ya katiba ambayo watarudi nayo vijijini na kuipitisha kwa wananchi ili waielewe kabla haijawa katiba rasmi na hatimaye wataizindua jumuiya iweze kufanya kazi yake lengo ni kuhakikisha kama wizara ya maji wadau wanaielewa sera , sheria na kuunda vyama vya watumia maji viweze kuhakikisha vinafanya kazi kwa niaba ya bonde kusaidia wizara kutunza mazingira na vyanzo vya maji.