September 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Tamasha la pili fahari ya Zanzibar kuzinduliwa

Na Mwandishi wetu,Timesmajira

Kampuni ya Airpay Tanzania imedhamini tamasha la pili la fahari ya Zanzibar linalotarajiwa kufanyika Septemba 20 hadi 27 mwaka huu huku Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Mwinyi akitarajiwa kuzindua tamasha hilo.

Akizungumza na waandishi wa habari Unguja Zanzibar Mkurugenzi Mtendaji wa Airpay, Yasmin Chali amesema kampuni hiyo ni mmoja kati ya wadau na mshirika mkuu katika tamasha la Pili la Fahari ya Zanzibar 2024, linalotarajiwa kufanyika katika Viwanja vya Dimani Fumba.
 
Amesema Airpay ni kampuni yenye mfumo wa kidijitali wenye lengo la kurahisisha mfumo wa malipo ya kifedha kwa watu wa kawaida, wafanyabiashara, na wajasiriamali wadogo.

Chali amesema kupitia ushirikiano wao na Wizara ya Nchi Afisi ya Rais, Kazi, Uchumi na Uwekezaji pamoja Wakala wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (ZEEA), wanalenga kuimarisha uwezeshaji wa kidijitali katika malipo na huduma nyingine za kifedha
 
Aidha amesema wanatambua na kuthamini jitihada za Serikali ya Zanzibar katika kuwezesha wajasiriamali kuanzisha na kukuza biashara zao na kwamba ushirikiano wao na serikali ni muhimu katika kuhakikisha malengo hayo yanatimia kwa ufanisi mkubwa.
 
“Kwa niaba ya timu ya Airpay, tunatoa pongezi za dhati kwa Rais Mwinyi, kwa jitihada zake za kuweka mazingira rafiki na yenye tija kwa wajasiriamali na wananchi kwa ujumla, tunatoa shukrani kwa ZEEA kwa ushirikiano mzuri unaoendelea, kuhakikisha mifumo yetu ya fedha inakidhi mahitaji ya wajasiriamali nakuchangia maendeleo ya kiuchumi ya Zanzibar, “ amesema

Naye Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Kazi, Uchumi na Uwekezaji, Sharif Ali Sharif amesema tamasha hilo litatoa fursa kwa wajasiliamali kutambulika zaidi katika masoko ya kimataifa pamoja na kukuza bidhaa zinazozalishwa nchini.

“Tamasha hili litatoa fursa kwa wajasilimali wazawa kushiriki na kupadilishana uzoefu na wengine kutoka nje ya nchi” amesema

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa ZEEA, Juma Burhan Mohamed amewakaribisha wajasiriamali wote wa Zanzibar kujitokeza kwa wingi kushiriki katika tamasha hilo.