March 8, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Ahadi za kampeni ya Mgombea Urais wa CCM,Dkt.Samia Suluhu Hassan 

Na Mwandishi  wetu,Timesmajira

Mgombea wa Urais wa CCM,Dkt. Samia Suluhu Hassan,ameendelea kuchanja mbunga kusaka kura za kuomba dhamana ya utumishi kwa watanzania katika nafasi ya Urais.

 Ambapo jana Agosti 3,2025 amefanya mikutano mikubwa ya kampeni katika

majimbo ya Tunduma na Vwawa mkoani Songwe. 

Dkt. Akiwa Tunduma aliwashukuru wananchi kwa kujitokeza kwa wingi kwenye

mkutano wa kampeni, na hasa vijana kwa mshikamano wao mkubwa.

Amewaeleza wananchi kuwa safari ya maendeleo itaendelea kwa kasi

zaidi endapo watamchagua tena kuongoza nchi katika kipindi cha

2025-2030.

Ameahidi kuendeleza sekta za elimu, afya, maji na umeme kwa kuongeza

shule, kuendeleza sera ya elimu bila ada, na kuongeza mikopo kwa

wanafunzi ili vijana wote wapate fursa ya masomo.

 Aidha, ameahidi kujenga vyuo vya VETA katika mkoa wa Songwe, ili vijana wapate ujuzi na kujiandaa kwa ajira na kujiajiri. Kuhusu afya, alisisitiza kuwa hospitali

mpya, vituo vya afya na zahanati zaidi vitajengwa ili wananchi wapate

huduma karibu na makazi yao.

Kwa upande wa maji, Dkt. Samia ameahidi kumaliza miradi mikubwa ya

maji, kwa lengo la kuhakikisha kila Mtanzania anapata maji safi na

salama, kufikia asilimia zaidi ya 90 upatikanaji vijijini na mijini. Vilevile,

alisema kuwa kila kaya itapatiwa huduma ya umeme na kuongeza

kuwa ahadi yake ya Bima ya Afya kwa Wote tayari imeanza kufanyiwa

majaribio, ambapo serikali itabeba gharama za matibabu kwa wale

wasio na uwezo.

Akizungumzia miundombinu, ameeleza kuwa maboresho makubwa

yaliyofanyika Bandari ya Dar es Salaam yameongeza tani ya mizigo

inayopita Tunduma, na sasa serikali imeanza kukarabati barabara kuu

ya TANZAM. 

Ameahidi kukamilisha kipande cha Igawa–Tunduma na Songwe–Tunduma (km 75) na kuendelea na vipande vilivyosalia,

sambamba na kuimarisha reli ya TAZARA ili iwe ya kisasa zaidi na iweze

kubeba mizigo kwa haraka.

Aidha Dkt. Samia,ameahidi kukamilisha ujenzi wa bandari kavu kubwa ya

ekari 1,800 eneo la Katenjele, kata ya Mpemba, ili kuondoa msongamano wa malori barabarani.

 Pia, barabara mbadala

zitajengwa, sambamba na maegesho ya kisasa na mizani mpya.

Amesisitiza pia kwamba atahakikisha nyaraka za mizigo zinachakatwa

mapema kabla ya kufika mpakani ili kupunguza muda wa kusubiri. Dkt.

Samia alisema atazungumza na Zambia kuhakikisha nao, kupitia

mamlaka ya mapato, wanafanya kazi saa 24 ili wananchi wapate

huduma kwa haraka.

 Dkt. Samia Kuhusu nishati, amewaomba wananchi wa Tunduma kumpa kura nyingi za ndiyo ili akamilishe mradi wa umeme mkubwa wa KV 730 kutoka Iringa, Njombe hadi Songwe, ambapo KV 430 zitatumika

Songwe na kV 300 zitaelekezwa Zambia.

 Amebainisha kuwa mazungumzo

ya kuuza umeme yameanza na kwa wakati huo huo serikali yake itaendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi majumbani ili kuboresha maisha ya wananchi.

Akiwa katika jimbo la Vwawa,Dkt. Samia Suluhu aliwahutubia

wananchi katika mkutano uliofanyika Vwawa. 

Katika mkutano huo

aliahidi kukamilisha ujenzi wa barabara muhimu ya Kamsamba na

kuhakikisha wilaya zote zinaunganishwa na barabara za lami hadi

makao makuu ya mkoa.

Kuhusu sekta ya kilimo, Dkt. Samia ameeleza kuwa changamoto ya

upatikanaji wa mbolea iko mbioni kutatuliwa kwani mbolea ya

kupandia tumbaku na mazao mengine tayari imeingia na ipo kwenye

hatua ya kusambazwa. 

Ametumia nafasi hiyo kupongeza wakulima kwa

mafanikio makubwa, akibainisha kuwa Tanzania imeshika nafasi ya pili barani Afrika kwa uzalishaji wa chakula, hususan mahindi, na kwamba

taifa lina kiwango cha asiimia  128 cha utoshelevu wa chakula. 

Amesema

mafanikio haya yamechochewa na mpango wa ruzuku ya pembejeo

unaotekelezwa na serikali ya CCM.

Kuhusu nishati, alibainisha kuwa umeme si changamoto kubwa tena

Songwe, lakini ataendelea na mkakati wa kujenga njia mpya ya

kusafirisha umeme yenye uwezo wa kV 730. Kati ya hizo, kV 430

zitatumika katika mikoa ya kusini, huku kV 300 zikielekezwa Zambia kama

sehemu ya mpango wa biashara ya nishati.

 Amesisitiza pia umuhimu wa

nishati safi na akaahidi kuialika sekta binafsi kushiriki katika kujenga vituo

vya kusambaza nishati hiyo.

Kwa upande wa vijana, aliahidi kuendeleza fursa kwao kupitia mikopo

ya elimu na ujenzi wa vyuo vya VETA katika mkoa wa Songwe.

Amesema kuwa ada na gharama za mafunzo hayo zitabebwa na

serikali, ili kuhakikisha vijana wote wenye nia na uwezo wa kusoma

wanapata nafasi ya kupata ujuzi na hatimaye ajira.