October 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mjumbe wa Kamati Kuu, Kassim Majaliwa, akizungumza wananchi wa Kata ya Nyamswa, wilayani Bunda, katika mkutano wa kampeni, uliyofanyika Komon’gwe, Septemba 19, 2020. Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu

Majaliwa:Watanzania chagueni viongozi wanaohubiri amani

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online, Mara

MJUMBE wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Kassim Majaliwa amewataka Watanzania wawachague viongozi wanaohubiri amani ikiwa ni moja ya tunu ya Taifa hili.

Ametoa wito huo jana jioni (Ijumaa, Septemba 18, 2020) alipokuwa akizungumza na wakazi wa kata Bunda Stoo, wilaya ya Bunda, mkoani Mara kwenye mkutano uliofanyika katika viwanja vya shule ya msingi Miembeni.

Mjumbe wa Kamati Kuu, Kassim Majaliwa, akizungumza wananchi wa Kata ya Nyamswa, wilayani Bunda, katika mkutano wa kampeni, uliyofanyika Komon’gwe, Septemba 19, 2020. Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu

Alikuwa akimuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dkt. John Pombe Magufuli, mgombea ubunge wa jimbo la Bunda Mjini, Robert Chacha Maboto, mgombea udiwani wa kata ya Bunda Stoo, Joseph Nyamangoko na wagombea udiwani wengine 13 wa kata za wilaya ya Bunda waliokuwepo kwenye mkutano huo.

Majaliwa alisema ni muhimu kwa wananchi kuchagua chama ambacho kitalinda amani ya nchi hii. “Amani ya nchi hii inaanza kuonekana kwa viongozi wenyewe wanapokuja kuomba ridhaa kwenu, sina mashaka mmeshaanza kuona na kujifunza ni kiongozi yupi ataleta amani katika nchi hii.”

Amesema kuwa Chama cha Mapinduzi kinaomba ridhaa ya Watanzania kwa awamu ya tano ya kipindi cha pili ili kuifanya Tanzania kuwa na amani na iendelee kuwa kimbilio kwa nchi zilizokosa amani.

Majaliwa ameongeza kuwa ni muhimu kupata kiongozi atakayeleta amani, maendeleo, mpenda mabadiliko, mpenda Watanzania na wanyonge wote; “na kwa sasa ni Rais Dkt. John Magufuli anayeweza kutekeleza hayo,” alisisitiza.

Majaliwa amesema kuwa Rais Dkt. Magufuli kwa kutambua umuhimu wa sekta ya mifugo na kilimo aliamua kuviacha vijiji 920 kati ya 970 viendelee na shughuli za malisho na kilimo kwenye maeneo ya hifadhi na eneo la kinga la mita 500.

Amefafanua kuhusu mafanikio yaliyopatikana kwenye sekta ya elimu ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya CCM ya 2015-2020, Mheshimiwa Majaliwa alisema sh. bilioni 4.9 zilitolewa kwa shule za msingi 100 za wilaya hiyo kwa ajili ya ukarabati, masuala ya utawala, michezo, mitihani na posho kwa maofisa elimu kata na walimu wakuu.

“Kwenye shule zenu za sekondari hapa Bunda, shilingi bilioni 1.8 zilitolewa kwa shule 17 kwa ajili ya fidia ya ada, chakula kwa shule za bweni na posho ya madaraka kwa wakuu wa shule.”

Ameelezea mfumo wa uboreshaji wa miundombinu ya shule wa Lipa Kutokana na Matokeo (EP4R) uliotekelezwa tangu 2015 hadi 2020, Mheshimiwa Majaliwa alisema sh. milioni 364.2 zilitolewa kwa ajili ya ukamilishaji wa miundombinu ya madarasa, vyoo na nyumba.

Amezitaja shule zilizonufaika na maboresho hayo kuwa ni shule za msingi Ikizu, Busore, Bigegu, Haruzale, Tingirima, Karukekere A, Rakana, Bunyunyi, Kasuguti, Nyabuzame, Kiloleri, ibwagalilo na Nyamitwebili.

“Shule za sekondari zilipatiwa shilingi milioni 667 kwa ajili ya ukarabati na ujenzi wa miundombinu ya shule ikiwemo maabara, madarasa, mabweni na vyoo kwa shule za Makongoro, Mwibara, Bulamba, Chisorya, Nyamag’uta, Hunyari, Nyeruma, Esperanto na Mwigundu,” amesema.

Kwenye sekta ya barabara, Mheshimiwa Majaliwa alisema wilaya ya Bunda imepatiwa sh. bilioni 46.5 ambazo zinatumika kujenga km. 56.4 za barabara ya Nyamuswa – Bunda – Bulamba kwa kiwango cha lami ikiwa ni awamu ya kwanza.

Amesema kiasi kingine cha sh. bilioni 2.9 kimetumika kutengeneza barabara kwenye sehemu korofi, madaraja na makaravati na matengenezo ya kawaida.