Na Mwandishi wetu,Timesmajira
Mashirika ya Umma nchini yameshauriwa kuendeleza ubunifu, wepesi na mageuzi ya kimkakati ili kuongeza tija na kuchochea maendeleo ya taifa, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuyawezesha mashirika hayo kuwa yenye ushindani na ufanisi mkubwa.
Wito huo ulitolewa jijini Arusha, Agosti 25, 2025, katika Mkutano wa Wenyeviti na Watendaji Wakuu wa Taasisi za Umma, uliowaleta pamoja washiriki zaidi ya 650.
Mkutano huo wa siku nne, uliofunguliwa rasmi Agosti 24 na Makamu wa Rais Dk. Philip Mpango, unalenga kuyawezesha mashirika hayo kuwa yenye ushindani na ufanisi mkubwa.
Afisa Mtendaji Mkuu wa Puma Energy Tanzania, Fatma Abdallah, amesema ni lazima mashirika hayo yaondokane na urasimu unaokwamisha kasi ya maendeleo na usambazaji wa huduma.
“Urasimu umekuwa ukichelewesha mambo kwa muda mrefu, lakini pia ni fursa ya kufikiria upya namna tunavyofanya kazi,”amesema.
Abdallah amesisitiza umuhimu wa kurahisisha mifumo ya utendaji na kuimarisha ushirikiano kati ya mashirika ili kuondoa ucheleweshaji na kuongeza uwajibikaji.
Amependekeza uundwaji wa mfumo endelevu unaojengwa kwa misingi ya utawala bora, uwazi wa kimkakati, uimara wa kibiashara, ubunifu, kanuni za ESG (Mazingira, Jamii na Utawala) na vipimo viwili vya utendaji (KPIs) vitakavyopima matokeo ya kifedha na ubora wa huduma kwa jamii.
“Utawala bora, mwelekeo wa kimkakati na ubunifu hujenga mashirika imara kwa ukuaji endelevu,” amesema.
Abdallah ametoa mifano ikiwemo mwitikio wa haraka wa kidijitali wa Wizara ya Afya wakati wa janga la COVID-19 na mfumo wa BRELA wa usajili wa biashara mtandaoni uliopunguza muda wa usajili kutoka wiki kadhaa hadi saa chache.
Ameeleza pia nguzo tano muhimu za mageuzi: dhamira ya uongozi, marekebisho ya sera na utawala, uwekezaji kwenye miundombinu ya kidijitali, nguvu kazi yenye wepesi na utamaduni wa utendaji unaolenga matokeo.
Kwa upande wake,Kenedy Komba, Mkurugenzi wa Huduma za Fedha Jumuishi kutoka Benki Kuu ya Tanzania, amebainisha jukumu la mashirika ya umma la kusawazisha ufanisi na utoaji wa huduma kwa wananchi.
“Mashirika ya umma yanapaswa kufanya kazi kwa ufanisi huku yakihakikisha wananchi wanapata huduma muhimu,” amesema.
Amesisitiza umuhimu wa kutumia teknolojia na uvumbuzi wa kifedha ili kuongeza uwazi na kupunguza urasimu.
Balozi Marie-Antoinette Rose-Quatre, Mtendaji Mkuu wa African Peer Review Mechanism, amesema Tanzania ina nafasi kubwa ya kuwa kitovu cha biashara na usafirishaji kwa Afrika Mashariki na Kusini kupitia mashirika ya bandari, usafirishaji na nishati.
“Mageuzi yanayoyabadilisha mashirika kutoka kwenye hasara hadi faida yanaweka mfano bora kwa bara zima,” amesema.
Amependekeza mashirika yaweke mikakati ya kupata mitaji kupitia masoko ya mitaji ya kikanda, pamoja na matumizi ya dhamana za serikali na hati fungani za kijani kwa miradi ya miundombinu na nishati.
“Tanzania inaweza kuongoza kwa mfano kupitia mageuzi ya kimkakati, utawala bora na ushirikiano wa kikanda,” ameongeza.

More Stories
Wanawake washauriwa kuchangamkia fursa za uchumi
Aida:Wanawake wakipata haki zote itapunguza migogoro
LGTI wanawake waadhimisha siku yao Ngorongoro