March 7, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Yas kutoa huduma kituo cha Biashara, Usafirishaji Afrika Mashariki (EACLC)

Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online

KAMPUNI ya Mawasiliano hapa nchini, Yas ni miongoni mwa Kampuni zitakazotoa huduma katika Kituo cha Biashara na Usafirishaji Afrika Mashariki (EACLC) kilichopo Ubungo, jijini Dar es Salaam.

Yas na Mixx by Yas ni mshirika rasmi na mtoa huduma wa kipekee wa mawasiliano na teknolojia ya kisasa kwa wafanyabiashara wote wanaohudumiwa na kituo hicho.

Kituo hicho kilifunguliwa rasmi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan Agosti 1,mwaka huu, ambapo kitakuwa na maduka zaidi ya 2,000.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Yas, Pierre Canton Bacara (katikati), akisalimiana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo (kulia), wakati wa hafla ya uzinduzi rasmi wa Kituo cha Biashara na Usafirishaji Afrika Mashariki (EACLC), iliyofanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam.

Aidha, kituo hicho cha kimataifa kilianza kujengwa kati ya mwaka mwaka 2022.

“Yas tunafurahia kuwa sehemu ya mradi huu wa kimkakati unaowapa fursa wafanyabiashara kukuza uchumi wa kidijitali,”.

Katika hafla ya ufunguzi wa kituo hicho, Afisa Mtendaji Mkuu wa Yas, Pierre Canton Bacara, alipata mafasi ya kukutana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo.

Mara baada ya kufungua kitua hicho, Rais Samia Suluhu Hassan aliwahimiza vijana kote nchini kutumia fursa za ajira zinazotolewa badala ya kulaumu kwamba Serikali haiwaoni.

“Tunaposema Serikali tunatengeneza mazingira kwa vijana, haya ndiyo mazingira yenyewe.

“Sasa ni nyinyi kutumia hizi fursa, kutumia kama mnavyoonyesha hapa, kutengeneza vitu tuwauzie nje. Msitulaumu Serikali hatuoni; kuona kwenyewe ndiyo hivi.

“Serikali haiwezi kuja kwa mmoja mmoja ikampa hivi, lakini tumetengeneza mazingira, myatumie,” amesema Rais Samia.