October 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mgombea Ubunge kupitia CCM Jimbo la Ilemela Dkt.Angeline Mabula akimnadi mgombea Udiwani wa chama hicho Kata ya Shibula Dede Swila kwenye mkutano wa kampeni za kuomba kura kwa wananchi uliofanyika shule ya msingi Masemele Kata ya Shibula Wilayani Ilemela Mkoani Mwanza. (Picha na Judith Ferdinand).

Dkt.Angeline: Chagueni viongozi wenye maono

Na Judith Ferdinand, TimesMajira Online, Mwanza

KAMPENI za ugombea Ubunge kupitia Chama cha Mpinduzi (CCM) Jimbo la Ilemela zimeendelea huku mgombea Ubunge kupitia chama hicho Dkt. Angeline Mabula akiwataka wananchi kuchagua viongozi wanaoweza kuwatumikia na kuwaletea maendeleo.

Akizungumza kwenye mkutano wa kampeni za uchaguzi uliofanyika katika uwanja wa shule ya msingi Masemele Kata ya Shibula, Wilayani Ilemela Mkoani Mwanza amesema, katika kipindi cha miaka mitano ya uongozi wake kupitia Rais John Magufuli katika Jimbo hilo wamefanikiwa kujenga shule mpya tatu za msingi na sekondari.

Lakini pia wametekeleza miradi mikubwa ya maji, urasimishaji wa makazi na umilikishaji wake ambao umefanyika kikamilifu huku jimbo hilo likiongoza kwa zoezi hilo kwa kipindi cha miaka mitatu mfululizo

“Niwaombe ndugu zangu mtuchague tena mimi binafsi kuwa mbunge wenu, Rais Magufuli na madiwani wanaotokana na CCM ili tukaendelee kuwaletea maendeleo na kuendeleza pale tulipoishi, hivyo msijaribu kuchagua viongozi ambao watajinufaisha wenyewe, chagueni ambao wapo tayari kuwatumikia na kuwaletea maendeleo mimi nipo tayari kuendelea kuwatumikia kwani kwa kipindi cha miaka mitano mambo mengi tumefanya,” amesema Dkt.Angeline.

Pia amewataka wananchi kutouza viwanja vyao kuholela na kuzingatia zoezi la umilikishwaji kwa faida yao ya sasa na vizazi vijavyo huku akiendelea kwa kusema kuwa ataendeleza michezo kama alivyokuwa ameanza katika kipindi cha uongozi wake awamu ya kwanza kupitia mashindano ya The Angeline Ilemela Jimbo cup.

Kwa upande wake Meneja Kampeni wa Jimbo la Ilemela Kazungu Idebe amewasisitiza wananchi hao kuwapuuza wanasiasa wasiokuwa na nia njema wanaohubiri chuki, utengano na kukwamisha maendeleo kwani CCM kupitia mgombea wake wa Urais Dkt John Magufuli na Serikali yake wametekeleza shughuli kubwa ya kuwaletea wananchi Maendeleo ikiwemo ukamilishaji wa miradi ya reli ya kisasa, mradi wa umeme wa Strigers Gorge, ununuzi wa ndege, ujenzi wa hospitali, zahanati na vituo vya afya.