September 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Timu kubwa zatakiwa kutambua vipaji ligi za mchangani

Na Esther Macha,TimesmajiraOnline,Mbarali

MBUNGE wa jimbo la Mbarali mkoani Mbeya,Bahati Ndingo amezitaka timu zinazoshiriki ligi kuu kufuatilia mashindano ya timu za mchangani ambazo zinaendelea wilayani humo ili kuweza kuwaona vijana wenye vipaji  na kuwasajili kwenye timu zao.

Ndingo amesema kuwa kuna vijana ambao wana uwezo mkubwa lakini hawaonekani popote hivyo timu kubwa zinazoshiriki ligi zikiwachukua vijana itakuwa sehemu  ya kupata ajira kupitia michezo hiyo.

Ndingo amesema hayo  Septemba 19,2024 wakati wa ufunguzi wa mashindano Bahati Cup 2024 yanayofanyika katika viwanja vya polisi kata ya Chimala wilayani hapa.

“Michezo ni ajira kwa hiyo hapa mmeona vipaji vinavyoendelea kwa hakika kazi nzuri na tumeona vipaji kubwa ni vema tualike timu kubwa ziendelee kuangalia ligi hii ili waweze kuwaona vijana wetu wenye vijana vipaji ambao wana uwezo mkubwa na kutoa mchango wao kwenye ligi kubwa na baadaye waweze kuonekana na kuwa sehemu ya kupata ajira ”amesema Mbunge huyo.

Aidha Ndingo amesema kuwa lengo la mashindano hayo kuwakutanisha vijana  pamoja na kuhamasisha kushiriki uchaguzi wa serikali za mitaa na kwamba jambo hilo ni muhimu na kutambua kuwa vijana walio ni wengi kutamani kutumia haki yao ya kikatiba vizuri kwa kuchagua viongozi ambao watawahitaji.

Aidha Ndingo amesema kamati ya ligi hiyo itakuwa Octoba 14, 2024 na mshindi wa kwanza atapata mil.5 na mshindi wa pili Mil.3, mshindi wa tatu mil.2 na mshindi wa nne mil.1 pia watakuwa na golipa  bora kwa kupatiwa kiasi cha sh.100,000 huku  mfungaji bora akizawadiwa kitita cha 100,000 na timu yenye nidhamu kupata  kujinyakulia zawadi.

Akizungumzia malengo ya mashindano hayo Mbunge Ndingo amesema kuwa yatakuwa yakiendeshwa kila mwaka na kuendelea kujipanga kuona ya kufikia kuna michezo mingine kwani kuna vipaji vimejitokeza kwa wanawake  kucheza mpira wa miguu wakati ufunguzi wa mashindano haya  kuna vipaji  vingi vimeonekana  na kuwa michezo yote wataifikia ili kuendelea kuibua vipaji ili  vijana wajisikie furaha kushiriki mashindayo hayo.

Hata hivyo Ndingo amewataka wazazi kuruhusu vijana kushiriki michezo kwani wakiwaacha kwenye vijiwe kwa muda mrefu wanaweza kwenda kwenye mambo  yasiyofaa hivyo kushiriki kwao kwenye michezo wanaepuka  vitu vingi visivyo na maadili kikubwa ni kufuatilia kama kweli wanafika wanakotakiwa na kusema kwa kiasi kikubwa michezo inasaidia kujiepusha na mambo mengi yasiyofaa katika jamii.

Ndingo ameeleza kuwa wilaya ya Mbarali ina tarafa mbili ambazo ni Ilongo na Rujewa hivyo kila tarafa itatoa timu 12, ambazo zitachuana kutokana na ukaribu wao na kutafuta mshindi wa pili na kwanza kutoka kwenye hizo tarafa ambapo zitakutana kwenye nafasi nne .

Mgeni Rasmi katika mashindano ya Bahati Cup2024 ,Mkuu wa Wilaya Mbarali  Kanali Maulid Surumbu amesema kuwa kupitia michezo vijana wataweza kujua afya zao na kufahamu changamoto katika afya na  vipaji vya vijana  pamoja  kujenga ushirikiano kujenga undugu na kuimarisha mshikamano jambo ambalo ni muhimu katika  kulinda ulinzi na usalama kwa wilaya ya mbarali.

Kanali Surumbu amesema kuwa kupitia mashindano hayo vijana wataonekana ili kuweza kupata fursa toka  timu kubwa zilizopo Tanzania wafike Mbarali kuchagua vijana kutoka Mbarali ambao wataonyesha vipaji vyao wakati mashindano hayo yatakapokuwa yakiendelea .

“Vijana muwe tayari kwa wale ambao watakuwa wamepata nafasi ya kucheza kwa nidhamu,fateni miongozo mliyofundishwa na walimu wenu makocha na pia muheshimu maamuzi yatakayotolewa na makocha wataongoonza michezo hiyo na maelekezo mengine na kwa kufanya hivyo mtaepuka changamoto za kukanyagana bila sababu,kuumizana,ili kufikia lengo la michenzo kuwa ni furaha”amesema Kanali Surumbu.

Mmoja wa wachezaji kutoka timu ya Chimala,Diof Peter amesema kuwa mashindano hayo ni mazuri kwa vijana yataibua vipaji  kwa vijana  na kusema malengo yake ni kufika mbali kwani hana kazi nyingine ambayo anategemea  katika kujiingizia  kipato hivyo mpira ni jitihada za mchezaji ikiwa atasikiliza viongozi pale anapopewa maelekezo.