September 27, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Rais Dkt.Samia ahimiza matumizi ya umeme kwa maslahi ya uchumi

Na George Mwigulu,Timesmajiraonline, Mlele.

RAIS Dkt.Samia Suluhu Hassan amehimiza matumizi ya umeme wa gridi ya taifa kwa maslahi ya uchumi utakao chochewa na uwekezaji wa viwanda na biashara katika Mkoa wa Katavi.

Amesema hayo leo,Julai 13, 2024 baada ya kukagua ujenzi wa moja ya vituo vya kupokea, kupoza na kusambaza umeme wa gridi ya taifa Inyonga wilaya ya Mlele utakapokea kutoka kituo kikuu Ubungo.

Uingizwaji wa umeme wa gridi ya taifa katika Mkoa wa Katavi unahusisha ujenzi wa vituo vya kupokea,kupoza na kusambaza umeme ambapo thamani thamani yake ni fedha Bilioni 48 na ujenzi wa njia ya umeme ambao umegharimu fedha Bilioni 116.

Rais Dkt Samia amesema kuwa nishati ya umeme ni tegemeo kubwa kwa uchumi wa mtu binafsi pamoja na viwanda vya uchumi mkubwa ambapo kwa umuhimu huo ilani ya uchanguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2020 ilibainisha mikakati ya kuhakikisha nchi inakuwana na umeme wakutosha.

“Tuliahidi kuhakikisha nchi inazalisha umeme wa kutosha ili kukidhi mahitaji ya kiuchumi na tuliahidi usambazaji wa umeme katika vijiji vyote na maeneo ya pembezoni,”amesema Rais Dkt Samia.

Rais Dkt Samia amesema “Kwa msingi huo nimekuja kukagua mradi wa kupoteza umeme Inyonga na nikiwa pale nimeona kazi nzuri iliyofanywa na kwamba mwenzi wa tisa Mkoa huu utatumia umeme wa gridi ya taifa na tunakwenda kuachana na majenereta ambayo yanatumia pesa nyingi kama Bilioni mbili kila mwenzi kuendesha jenereta ndani ya Katavi”

Ameweka wazi kuwa ni muhimu kwa wananchi pindi umeme wa gridi ya taifa utakapoanza kuwaka kuutumia ipasavyo “Mbali na kutunza mradi huu tuumieni umeme kwa masirahi ya kiuchumi anayweza kufungua saluni ya kunyoa nywele na aweke,anayeweza kuchoma vyuma na kutengeneza madirisha na aweke…umeme wa uhakika usiokata wawekezaji bila shaka pia watakuja na shuguri za uwekezaji zitaendelea”

Katika hatua nyingine ameitaka Wizara ya Nishati, Naibu Waziri Mkuu ambaye ni Waziri wa Nishati na Shirika la Umeme Tanesco kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati sambamba na shughuli zingine ya usambazaji na uuganishaji wa umeme kwenye taasisi na kwenye vyumba za watu Tanesco wanafanya kazi hiyo.
Aidha amewashukuru baadhi ya wananchi wa Mkoa wa Katavi waliokubali umeme upite na baadae fidia ifuate kwani kitendo hicho ni cha kizalendo na amewahakikishia wote waliopo kwenye maeneo ya mradi fedha Bilioni nne zilizobakia za fidia watalipwa.

Mkurugenzi Mtendaji wa Tanesco, Mhandisi Gissima Nyamo Hanga awali akisoma taarifa ya utekelezaji wa mradi huo amesema kuwa ujenzi kituo cha kupokea,kupoza na kusambaza umeme wa gridi ya taifa umekamilika kwa asilimia na 97 na njia ya umeme kwa asilimia 63.

Mhandisi Gissima vilevile amewahikikishia wananchi wa mkoa wa Katavi kwamba ujenzi wa mradi huo utakamilika kwa wakati ifikapo mwezi wa tisa mwaka huu.

Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Mwanamvua Mrindoko amesema kuwa mkoa huo umefikiwa na umeme wa REA katika vijiji 172 na kwa kuwa umeme wa gridi ya taifa umebaki asilimia ndogo kukamilika tatizo la umeme litakuwa limemalizika.