September 28, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali yatoa bil.2 ujenzi wa barabara ya lami Mbalizi Shigamba

Na Esther Macha,TimesmajiraOnline,Mbeya

WAKALA ya barabara(TANROADS)mkoa wa Mbeya umesema kuwa tayari serikali imetenga Bil.2 kwa ajili ya  ujenzi wa kilometa 52, za barabara kiwango cha Lami  kutoka Mbalizi hadi Shigamba Umalila wilaya ya Mbeya.

Imeelezwa kuwa serikali chini ya Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan imetoa kiasi hichi cha fedha kwa hatua za awali ambapo ujenzi huo unatarajiwa kuanza hivi karibuni.

Kauli hiyo imetolewa na Kaimu meneja wa TANROADS,mkoa wa Mbeya Mhandisi,Kamokene Sanke wakati akizungumza na wananchi wa kijiji cha Sanje kata ya Santilya wilayani Mbeya wakati wa ziara ya Mbunge wa Mbeya vijijini ,Oran  Njeza kusikiliza kero za wananchi.

“Mheshimiwa Rais tayari ametoa fedha shilingi Billion mbili na sasa tuko kwenye hatua za mwisho za manunuzi ili kuanza utekelezaji wa mradi wa kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami huku akiwaomba wananchi kuendelea kujenga imani na viongozi wao kuwa barabara hiyo itajengwa”amesema Mhandisi Sanke.

Kwa upande wake Kaimu Meneja Wakala wa barabara mjini na vijijini Wilaya ya Mbeya (TARURA) Arcad Tesha amesema barabara inayoanzia njiapanda ya Soweto hadi Sanje ina urefu wa kilomita nane na kwa kuanza kuanzia juma lijalo wataanza kuweka kifusi kwenye eneo la kilomita tatu za barabara hiyo.

Pia TARURA wilaya ya Mbeya inaelekeza nguvu kwenye ujenzi wa daraja linalounganisha vijiji vya Sanje na Itizi kutokana na daraja hilo kutopitika na kuhusu barabara nyingine iliyolalamikiwa amesema haipo kwenye mfumo wa mtandao wa barabara na pamoja na hayo TARURA haitanyamaza.

Pia barabara ya Itizi Sanje Jojo yenye urefu wa kilomita 15 imeelezwa kuwa ni kero hivyo TARURA imeeleza kuishughulikia kuhakikisha inapitika.

Mbunge wa Mbeya vijijini , Oran Njeza amesisitiza TARURA kutimiza matakwa hayo ya wananchi ili kuwasaidia kutokana na kutokuwa na miundombinu rafiki ombi ambalo pia amelielekeza kwa wahandisi wa maji kiu yake kuu ikiwa ni kuona wananchi wake wanapata huduma ya maji safi.

Kwa upande wake Beatrice Urio ambaye ni ofisa kutoka ofisi ya mipango Halmashauri ya Mbeya, amesema kwa niaba ya mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri hiyo kuwa Serikali ipo ili kuwatumikia wananchi hivyo wataendelea kutekeleza miradi mbalimbali kwa maendeleo ya wananchi.