September 28, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Maafisa Ustawi,Maendeleo elimisheni jamii elimu ya malezi na makuzi

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma

KAIMU Katibu Tawala wa Mkoa wa Dodoma Mhandisi Happiness Mgalula amewataka Maafisa Ustawi wa Jamii na Maafisa Maenseleo ya Jamii kuelimisha jamii kuhusu malezi  na makuzi hasa kwa watoto wenye umri wa sifuri hadi miaka minane.

Akifungua kikao cha tathimini cha  malezi,makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto kwa ajili ya utekelezaji wa Programu Jumuishi ya Malezi,Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto (PJT-MMMAM) mkoa wa Dodoma , Mhandisi Mgalula amesema katika eneo la malezi bado lina changamoto huku akisema kada hiyo ndiyo inayoweza kuisaidia jamii kwa kutoa elimu sahihi .

“Hii ni kada muhimu kwa maendeleo na ustawi wa watoto nchini,hivyo katika utekelezaji wa majukumu yenu muisaidie jamii kuelimisha hasa katika malezi na makuzi ya watoto wadogo ili waweze kuwa na ukuaji timilifu.”alisema Mhandisi Mgalula na kuongeza kuwa

“Ukiangalia huko kwenye jamii zetu hadi sasa bado kuna watoto wanaokosa fursa ya elimu na wazazi wao hawajali kitu,Maafisa Ustawi na Maendeleo ya Jamii ndiyo wa kuelimisha jamii ili watoto hao wasome maana kupitia ninyi changamoto za kijamii za malezi na makuzi ya watoto zitapata majawabu.”

Awali ,Afisa Ustawi wa Jamii  wa Mkoa wa Dodoma Josephine Mwaipopo amesema kikao hicho kimejumuisha wataalam wa Ustawi na Maendeleo ya Jamii kutoka Halmashauri nane za mkoa huo ambao kwa pamoja wanashirikiana katika utekelezaji wa PJT-MMMAM .

Amewahimiza wataalam hao kila mmoja kwa nafasi yake kuifanyia kazi Programu hiyo kutokana na umuhimu wake wa kutaka jamii iwe na malezi chanya kwa watoto ili wawe na ukuaji timilifu huku akiwasihi kutoa taarifa sahihi za utekelezaji wa Program ya MMMAM.

Vile vile amewataka wataalam hao kuhakikisha taarifa hizo za kila robo mwaka zinapita kwa wakurugenzi wa halmashauri na kuwajulisha kwamba baada ya hapo inaenda mkoani na kisha inapelekwa Ofisi ya Rais,Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI).

Akiwapatisha wataalam hao kwenye PJT-MMMAM Mkurugenzi wa Shirika lisilo la Kiserikali la Action for Community Care ambalo linatekeleza mradi wa Mtoto Kwanza kwa mkoa wa Dodoma unaopelekea utekelezaji wa PJT-MMMAM  Pendo Maiseli amesema malezi na makuzi ya watoto wa umri wa sifuri mpaka miaka minane kuna maeneo matano muhimu ya kuzingatiwa ambayo ni Afya bora,Lishe ya kutosha,malezi yenye mwitikio,ujifunzaji wa awali na ulinzi na usalama wa mtoto.

Aidha kikao hicho kimeazimia kukabiliana na changamoto zilizopo katika utekelezaji wa programu hiyo ikiwemo ya upatikanaji wa habari kwa kumwandikia  barua mwandishi kinara wa habari za MMMAM mkoani humo kwa ajili ya kumtambulisha kwa wakurugenzi wa Halmashauri.

Akisoma maazimio hayo Afisa Ustawi wa Jamii wa wilaya ya Bahi Songoro Msongo amesema  kikao kimeazimia kuhakikisha taarifa za wataalam zinahusisha na bajeti ya mwaka wa fedha ujao kwa ajili ya utekelezaji  wa programu,baafhi ya wakurugenzi hawaelewi Programu ya MMMAM lakini pia bado kuna halmashauri hazijafanya makabidhiano kutoka kwa maafisa Maendeleo kwenda kwa Maafisa Ustawi wa Jamii na kutakiwa kufanya hivyo.

Akihitimisha kikao hicho Afisa Ustawi wa Jamii mkoa wa Dodoma Amina Mafita amewataka wataalam hao wafanye kazi kwa kushirikiana katika shughuli mbalimbali kuwezesha utekelezaji wa Prigramu.

“Kama ambavyo mara nyingi tumeona kwamba bajeti ni changamoto,kwa hiyo mnapaswa kutumia rasilimali chache zilizopo katika halmashauri zetu katika utekelezaji wa Programu ya MMMAM ,lazima tufanye kazi hii kwa weledi ili ifikapo mwisho wa utekelezaji wake 2025/2026 mkoa wa Dodoma uwe kinara  katika kuitekeleza PJT-MMMAM.”amesema Mafita