October 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wadau waiomba Serikali kurejesha mchakato wa Katiba Mpya

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

WADAU mbalimbali walioshiriki katika mjadala wa wazi uliondaliwa na Chama Cha Wanasheria Tanganyika (TLS) wameiomba Serikali kurejesha mchakato wa Katiba Mpya ambao umekwama kwa muda mrefu.

Wakizungumza Jijini Dar es salaam katika mjadala huo uliojikita juu ya mchakato wa katiba mpya wamesema sasa ni wakati muafaka hivyo serikali inapaswa kurejesha mchakato huo .

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Sera za Kijamii Zanzibar, ambaye pia alikuwa Mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba, Mohammad Yussuf Mshamba alisema
ni muda muafaka wa kuanza kwa mchakato huo ambao ulikwama kwa takribani miaka 10.

Amesema urejeshaji wa mchakato wa katiba ni suala linalohitaji utayari wa serikali hivyo aliiomba Serikali iludishe mchakato wa rasimu ya warioba.

Alisisitiza kuwa ni vyema Mchakato usihusushe wanasiasa na badala yake ushishirikishe zaidi wananchi ili waweze kujitokeza kwa wingi.

“Ni lazima kuwe na njia ambayo itasaidia kupata maoni ya wananchi ambapo hapo ni suala la utayari tu serikali na Chama kilichopo madarakani, inawezekana chama kinataka twende kwenye Uchaguzi ujao tukiwa bado hatujapata Katiba Mpya,” amesema

Akichangia mjadala huo, Mwanafunzi wa Chuo cha Sheria, Queen Elizabeth Francis alisema kupatikana kwa Katiba Mpya ndo suluhisho kwa Nchi na itaondoa changamoto mbalimbali zilizopo katika Katiba iliyopo ya mwaka .

“Naamini Katiba Mpya itakwenda kuleta suluhisho katika nyanja mbalimbali nchini, kwanza ihusisha wananchi kwa ujumla katika makundi tofauti tofauti waweze kutoa maoni yao tofauti na ile ya mwanzo ambayo imepitwa na wakati,” amesema Francis

Awali Akifungua mjadala huo, Mkurugenzi Mtendaji wa TLS, Mariam Othuman amesema wameshafanya mijadala hiyo katika Mkoa wa Arusha, Mwanza na Mbeya na kiu kubwa ya wananchi ni kupatikana kwa Katiba Mpya.

“Tangu tumeanza kufanya hiyo mijadala hii, maoni ya wananchi ni kwamba wanataka Katiba Mpya kwani wameona hii iliyopo ina mapungufu na inahitaji mabadiliko. Kwahiyo wote ukiangalia mrengo wao nadhani ni wakati muafaka kwa Tanzania kupata Katiba Mpyaa”amesema Othuman

Aidha alisisitiza kuwa kabla ya mabadiliko ya Katiba Mpya lazima wananchi waelewe kwamba hii iliyopo, isije kuwa wanahitaji Katiba Mpya lakini hii iliyopo hawajui ina kitu gani.

“Kwa sasa sisi TLS tunajielekeza katika kuwaelimisha kwanza, na kisha kuchukua maoni yao,” amesema.Othuman