October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akizungumza na mke wa Marehemu Balozi Job Lusinde, Mama Sara Lusinde aliyekaa katikati mwenye kilemba cheupe mara baada ya kuwasili kwa ajili ya kutoa pole nyumbani kwa Marehemu Balozi Lusinde Uzunguni jijini Dodoma.

Magufuli afariji familia ya Marehemu Balozi Lusinde

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online, Dodoma

RAIS John Magufuli, amekwenda kutoa pole kwa familia ya Balozi Mstaafu Job Lusinde aliyefariki dunia Julai 7,mwaka huu. Msiba wa Balozi Mstaafu Lusinde upo nyumbani kwake Kilimani Jijini Dodoma.

Rais Magufuli ambaye ni Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) alikwenda nyumbani hapo akitokea Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete Jijini Dodoma ambako ameongoza Kikao cha Kamati ya Maadili na Usalama na Kikao cha Kamati Kuu ya CCM.

Akiwa nyumbani kwa Marehemu Balozi Mstaafu Lusinde, Rais Magufuli alikutana na Mjane wa Marehemu, Sara Lusinde, ndugu, jamaa na marafiki wa Marehemu ambapo ameeleza  kuguswa na kifo cha Balozi Mstaafu Lusinde na kwamba daima atamkumbuka kwa mchango wake alioutoa akiwa Waziri wa Ujenzi, ushauri wake mzuri na moyo wake wa upendo na ukweli.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiandika kwenye kitabu cha Maombolezo kufuatia kifo cha aliyewahi kuwa Waziri katika Baraza la kwanza la Mawaziri la Serikali ya Awamu ya kwanza chini ya Mwalimu Julius Nyerere Marehemu Balozi Job Lusinde aliyefariki katika Hospitali ya Taifa Muhimbili jijini Dar es Salaam.

Rais Magufuli ameeleza kuwa wakati wa utumishi wake Balozi Mstaafu Lusinde alikuwa mzalendo wa kweli, mchapakazi na aliyetetea maslahi ya Tanzania nje ya nchi, na kwamba hata alipostaafu aliisemea vizuri Dodoma.

Amewataka wafiwa wote kuwa wastahimilivu na kumpuzisha salama hapo leo atakapozikwa.