September 24, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waganga Wafawidhi wasaini mkataba wa uwajibikaji

Na Israel Mwaisaka, TimesMajira Online, Rukwa

MGANGA mkuu wa mkoa Rukwa Ibrahimu Isaac amewataka waganga wafawidhi wa vituo vya kutolea huduma za afya kusimamia utoro kazini ikiwa ni pamoja na ulinzi wa vifaa tiba katika vituo vyao ikiwa ni pamoja na kufunga CCTV Camera kwenye vituo vyenye mali nyingi ili kulinda mali hizo za serikali.

Akizungumza na Waganga Wafawidhi wa vituo vya kutolea huduma za afya wilayani Nkasi katika ukumbi wa mkurugenzi mtendaji wa wilaya amesema kumekuwepo na utoro wa reja reja kazini ambapo hata vituo katika baadhi ya maeneo uchelewa kufunguliwa na kusisitiza utunzaji wa vifaa tiba maana kumeibuka wimbi wa wizi wa vifaa tiba katika maeneo mbalimbali Nchini.

Alisema Wananchi wanazihitaji sana huduma za afya hivyo ni lazima zitolewe kwa weredi mkubwa na kuhakikisha miundo mbinu iliyowekwa na serikali inatumika vizuri katika kuboresha huduma za afya katika vituo wanavyofanyia kazi.

Pia amewataka Waganga hao wafawidhi kuwa wabunifu katika utoaji wa huduma kwa kuongeza kutoa huduma nyingi za kiafya ili kuweza kuongeza mapato kwenye vituo vyao.

Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya Nkasi Pankrasi Maliyatabu kwa upande wake amewataka watumishi hao wa afya kuacha kuwa watu wa malalamiko na manung”uniko na kutii maagizo kutoka juu ili kuweza kuleta tija na kubwa serikali inataka huduma hizo za afya zitolewe kwa ubora na Wananchi wanufaike.

Alisema kuwa wakati serikali ikipanga ikama ya watumishi wake katika sekta hiyo ya afya ulazimika kufanya uhamisho wa Watumishi na kuwa sasa kimeibuka kitu kisicho kizuri kwa baadhi ya watumishi kugoma kuhama wakipata barua za uhamisho na kuwa huo ni utovu wa nidhamu na kuwa sasa yeyote atakaegoma watamchukulia hatua kali za kinidhamu kwani kufanya hivyo ni kosa.

Mwenyekiti huyo wa halmashauri amedai kuwa mtumishi anapoajiliwa moja ya sharti lake ni kwenda kufanya kazi eneo lolote atakalopelekwa na mwajili wake na kuhoji kuwa huo ujasili wa kumgomea mwajiri wanaupata wapi wakati wanajua kabisa kuwa wanavunja sheria za utumishi.

Awali kaimu mganga mkuu wa wilaya Josepha Joseph alidai kuwa mkataba huu utakua baina ya timu ya usimamizi na uendeshaji wa huduma za afya ngazi ya halmashauri na timu ya usimamizi wa huduma za afya ngazi ya kituo,mkurugenzi mtendaji wa halmashauri,mganga mkuu wa wilaya na mwanasheria kuthibitisha kuwa mkataba huo umehalalishwa kisheria.

Alisema kuwa mkataba huo ni sehemu ya uboresheni wa huduma za afya na kuwa atakaekwenda kinyume na mkataba huo atafikishwa mbele ya vyombo vya kisheria na ndiyo maana mikataba hiyo inasainiwa mbele ya Mwanasheria.

Mganga mkuu wa mkoa Rukwa Ibrahimu Isaac akizungumza na Waganga Wafawidhi wa vituo vya kutolea huduma huduma za afya wilayani Nkasi wakati wakisaini mikataba ya utekelezaji wa majukumu yao kwa weledi
Waganga Wafawidhi wa vituo vya kutolea huduma za afya wakisaini mikataba ya utekelezaji wa majukumu yao