September 24, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Elimu ya ukimwi yachangia maambukizi mapya kupungua

Na Israel Mwaisaka, TimesMajira Online, Nkasi

KUFUATIA elimu inayotolewa na Wataalamu wa afya juu ya kukabiliana na ugonjwa wa Ukimwi wilayani Nkasi mkoani Rukwa imepelekea maambukizi mapya kupungua baada ya watu wengi kujitokeza kupima na kujua hari zao na kuchukua hatua za haraka pale wanapobainika kuwa na Virus hivyo.

Katika taarifa iliyotolewa na mratibu wa Ukimwi wilayani Nkasi Lucas Mhigi kwenye maadhimisho ya siku ya Ukimwi jana ni kuwa kasi kubwa ya watu wanaojitokeza kupima afya ni kubwa na kurahisisha mapambano ya kukabiliana na ugonjwa huo ikiwa ni pamoja na kuhakikisha Waathirika wazitumia vyema dawa za kufubaza Virusi vya Ukimwi .

Alisema kuwa katika kufikia malengo ya 95 tatu ,lengo la kwanza ni upimaji wa VVU ambapo wamefanikiwa kufikia asilimia 98,Matumizi ya dawa wamefikia asilimia 98.3 na lengo la mwisho ni la upungufu wa Virus mwilini kufikia asilimia 97.

Jumla ya Wananchi 29,668,wamejitokeza kupima ikiwa Wanawake ni 15,748 na Wanaume 13,920 kwa mwaka 2021/2022 waliokutwa na maambukizi ni 920 ,wanawake 529 na Wanaume 391,waliofanyiwa tohara jumla 5,212 kwa mwaka wa 2021/2022,hari ya Watoto waliopata huduma jumla yao ni 529,wa kiume ni 198 na wa kike ni 331 na hii inaonyesha kuwa jamii kwa sasa imekua na mwamko wa kujua hari zao za afya.

Amedai kuwa mafanikio hayo yametokana na ushirikiano mkubwa kati ya serikali na mashirika yasiyo kuwa ya kiserikali ambayo ni Waterleed,Mkapa foundation,Shdepha Nkasi,CEELS,Nkango,HIMA na Wamanka na kuwa juhudi hizo zinaendelea kufanyika ili kufikia mwaka 2030 kusiwepo na maambukizi mapya ya VVU wala vifo vitokanavyo na Ukimwi.

Mkuu wa wilaya Nkasi Peter Lijualikali kwa upande wake alipongeza jitihada hizo zinazofanywa na idara ya afya kwa kushirikiana na wadau na kuwa jitihada hizo ziendelee na wao kama serikali watajitahidi kusaidia jitihada hizo ili kuweza kuyafikia malengo ya kuondoa kabisa maambukizi mapya sambamba na vifo vitokanavyo na Ukimwi.

Alisema kinachofurahisha sasa ni kuona wale wanaotumia dawa za kufubaza Virus vya Ukimwi hawakimbii kama ilivyokuwa hawali na kuwafanya kuwa na afya njema na kuwahimiza kuendelea kutumia dawa hizo huku akiwasihi wataalamu wa afya kuwatembelea mara kwa mara Waathirika na kuwahimiza kuendelea kutumia dawa hizo

Mmoja wa mashuhuda anayeishi na Virus vya Ukimwi alidai kuwa yeye baada ya kutambua kuwa amepata Virus vya Ukimwi na baada ya kupata ushauri wa wataalamu aliamua kuwa mwaminifu kwenye matumizi ya dawa za kufubaza ugonjwa huo na kuwa imemfanya kuwa na afya njema na kuwa sasa anaishi na Virus hivyo kwa zaidi ya miaka kumi sasa.

Hivyo amewataka watu kuendelea kujitokeza na kupima afya zao mara kwa mara na kuwa hilo litawasaidia kuanza kutumia dawa mapema pale watakapobainika kuwa na Virus hivyo na kwa wale wanaotumia dawa wasiache kwani huo ndiyo uhai wao na kuacha kabisa kufanya ngono zembe zitakazopelekea maambukizi mapya ya VVU.

Maadhimisho hayo ya Ukimwi mwaka huu yamebeba ujumbe usemao “JAMII IONGOZE KUTOKOMEZA UKIMWI”

Mkuu wa wilaya Nkasi Peter Lijualikali akizungumza kwenye maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani.
Wataalamu wa afya wakitoa elimu juu ya matumizi sahihi ya Condomu kwenye maadhimisho ya siku ya ukimwi duniani
Mwanachama wa Redcross Hamisi Monero akichangia damu siku ya ukimwi duniani