October 1, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Othmani aungana na wananchi katika mazishi Mhe. Habibu

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Mheshimiwa Alhaj Othman Masoud Othman, leo Machi 03, 2023 amejumuika na Wananchi na viongozi mbali mbali wa Serikali, Dini na Siasa, katika Maziko ya Marehemu Habibu Ali Mohammed.

Marehemu Habibu ambaye hadi kifo chake alikuwa Muwakilishi wa Jimbo la Mtambwe kisiwani Pemba kupitia Chama cha ACT Wazalendo, amefariki Dunia Alfajir ya Machi 03, huko jijini Dar es salaam alipokuwa akipatiwa matibabu baada ya kuugua kwa muda mfupi, na amezikwa Kijijini kwao Uondwe – Mtambwe, Mkoa wa Kaskazini Pemba.

Marehemu Habibu ameacha Familia ya Mke mmoja (1) na Watoto sita (6).

Miongoni mwa Viongozi waliojumuika katika Maziko hayo ni Mhe. Hemed Suleiman Abdulla, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar; Ndugu Zitto Zuberi Kabwe, Kiongozi wa Chama cha ACT Wazalendo; Babu Juma Duni Haji, Mwenyekiti wa Taifa wa ACT Wazalendo; Mhe. Zubeir Ali Maulid Spika wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar;
Mawaziri, Wawakilishi, Wabunge na Watendaji mbalimbali wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wakiongozwa na Mhe. Omar Said Shaaban, Waziri wa Biashara na Maendeleo ya Viwanda hapa Visiwani.

Kabla ya hatua hiyo, Mwili wa Marehemu umeandaliwa katika Masjid Maamur Jijini Dar es Salaam; ameswaliwa katika Msikiti wa Jamii Zinjibar Unguja; umewasilishwa katika Baraza la Wawakilishi, na hatimaye kusafirishwa kisiwani Pemba, kwaajili ya Mazishi.

Mungu Ailaze Roho ya Marehemu Mahala Pema Peponi, Amin!

Mwisho