September 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watahiniwa 2,194 wa darasa la saba wafutiwa matokeo yao

Na Penina Malundo 

BARAZA la Mtihani nchini(NECTA) imesema  matokeo ya Mtihani wa kumaliza Elimu ya Msingi (PSLE)2022 yanaonyesha kuwa na ufaulu wa watahiniwa katika masomo yote uko juu ya wastani isipokuwa kwa somo la Kiingereza. 

Huku ikisema takribani matokeo ya Watahiniwa 2,194 sawa na asilimia 0.16 ya watahiniwa 1,350,881 waliofanya  mtihani matokeo yao yamefutwa  baada ya kubainika kufanya udanganyifu katika Mtihani huo kwa mujibu wa Kifungu 30(2)(b) cha Kanuni za Mitihani 2016 kikisoma pamoja na Kifungu cha 5(2) (i) na (j) cha sheria cha Baraza la Mitihani Sura ya 107 huku Watahiniwa 179 walizuiliwa  matokeo yao kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo kuugua,kupata matatizo na kushindwa kufanya mitihani kwa masomo yote au baadhi ya masomo.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam na Kaimu Katibu Mtendaji   wa Baraza hilo,Athumani Amasi wakati akitangaza taarifa ya matokeo ya Mtihani wa Kumaliza Elimu ya Msingi (PSLE),Oktoba 2022,amesema katika matokeo ya mwaka huu takwimu zinaonyesha kuwa idadi ya ufaulu kwa watahiniwa   imeongezeka kwa asilimia 18.24 kwa watahiniwa 165,600 ukilinganisha na mwaka 2021.

Amesema jumla ya watahiniwa 1,384186 wa Shule za Msingi walisajiliwa kufanya mtihani huo wakiwemo wasichana 723,027 sawa na asilimia 52.23 na wavulana 661,159 sawa na asilimia 47.77 huku  watahiniwa wenye mahitaji maalum walikuwa 4,221 sawa na asilimia 0.30.

“Watahiniwa 1,350,881 sawa na asilimia 97.59 ya waliosajiliwa walifanya mtihani kati yao wasichana  walikuwa 709,556 sawa na asilimia 98.14 na wavulana walikuwa 641,325 sawa na asilimia 97.00,Watahiniwa 33,305 sawa ma asilimia 2.41 hawakufanya mtihani kutokana na sababu mbalimbali, zikiwemo utoro na ugonjwa,”amesema

Akizungumzia Shule zilizofungwa,amesema vituo vya  Mtihani 24 sawa na asilimia 0.13 ya vituo 17,935 vya mitihani vilivyothibitika kupanga na kufanya udanganyifu katika Mtihani  wa kumaliza Elimu ya Msingi  mwaka 2022 kwa mujibu wa kifungu 4(8) cha kanuni za Mitihani mwaka 2016 hadi baraza litakapojiridhisha kuwa ni salama kwa uendeshaji wa mitihani ya Kitaifa.

Akitaja vituo hivyo ni pamoja naShule ya Msingi  Kadama Halmashauri ya Chato mkoani Geita ,Shule ya Msingi Rweikiza Manispaa ya Bukoba mkoani Kagera,Shule ya Msingi  Kilimanjaro  Halmashauri ya Arumeru,Shule ya msingi  Sahare Jiji Tanga,St.Anne Marie  Halmashauri ya Ubungo Dar es Salaam,Ukerewe Halmashauri ya Ukerewe Mwanza.

Shule nyingine ni Shule ya msingi Peaceland Halmashauri ya Ukerewa mkoani Mwanza,Shule ya msingi Karume Manispaa ya Bukoba  Kagera ,Al-Hikma iliyopo Jiji la Dar es Salaam,Kazoba Halmashauri ya Magu mkoani Mwanza,Busara  Halmashauri ya Magu Mwanza ,Jamie manisapaa ya Bukoba Kagera,Winners Jiji Mwanza,Musabe Jiji la Mwanza ,Elibasene iliyopo Tunduma ,High Challenge Halmashauri ya Jiji Arusha,Tumaini Iliyopo Halmashauri ya Sengerema ,Olele iliyopo Mwanza,Mustlead Halmashauri ya Chalinze ,Moregan Halmashauri ya Tarime ,Leaders Halmashauri ya Rorya mara ,kivulini iliyopo jiji ya mwanza  na Mtakatifu Severine iliyopo halmashauri ya Biharamulo Kagera.