April 30, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Byabato:Serikali imejipanga kuondoa matumizi ya mkaa na kuni nchini,kulinda uhifadhi wa mazingira

Na Zena Mohamed,Timesmajiraonline,Dodoma.

NAIBU Waziri wa Wizara ya Nishati Stephen Byabato amesema Wizara hiyo imejipanga vyema kuhamasisha jamii matumizi ya Nishati ya kupikia majumbani kwa watu wa Vijijini na mijini na kuondokana na matumizi ya mkaa na kuni ili kulinda uhifadhi wa mazingira.

Byabato amesema hayo jijini hapa leo  katika viwanja vya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  kwenye maonyesho ya shughuli mbalimbali za wizara hiyo yanayolenga kujibu maswali yanayohusu wizara hiyo ambapo ameeleza kuwa Nishati hiyo ya kupikia ni rahisi na inaweza kutumiwa na kila mtu .

“Serikali kupitia REA kwa mwaka wa fedha unaokuja imetenga jumla ya shilingi Trillion  6 na bilioni 500 kukidhi mahitaji ya mradi huo na kwamba mahitaji yatagawanywa kulingana na uhalisia wa vijiji husika,

“Na tumeshajipanga Kujenga vituo vitano vya gesi Kwa ajili ya kutandaza mabomba kuelekea majumbani,Mpango ni mkubwa zaidi wa kuongeza Kasi ya gesi ya kupika na kuwahudumia wananchi wengi zaidi sio mjini pekee Bali hata vijijini,”amesema.

Amefafanua kuwa kwa kuanza mradi huo ulianzia majaribio kwa Mkoa wa  Mtwara ambapo nyumba 600 hadi sasa zinatumia Nishati ya gesi Kwa matumizi za nyumbani Kisha kuongeza nyumba nyingine 400 na kufisha idadi ya nyumba 1000 ambazo zimefikiwa na gesi ya kupika majumbani hadi sasa.

Amesema baada ya kufanikiwa Kwa mradi huo,mradi unaofuata ni Dar Es Salaam ,Pwani,Lindi,Dodoma kufuatia  na mikoa mingine.

Naibu waziri huyo pia amesema katika kuboresha zaidi mahitaji hayo wamepanga kujenga vituo vitano vya gesi kwa ajili ya kutandaza mabomba kuelekea majumbani.

“Mpango ni mkubwa zaidi wa kuongeza kasi ya gesi ya kupika na kuwahudumia wananchi wengi zaidi sio mjini pekee bali hata vijijini,tunafanya hivi ili kuwapa unafuu wananchi na kuhifadha mazingira,”alisema

Katika hatua nyingine Naibu waziri huyo wa Nishati amesema katika kusambaza huduma za nishati ya gesi,tayari huduma hiyo inatumika kwenye magari na kueleza kuwa hadi sasa kuna zaidi ya magari 600 yanatumia gesi .

“Tulianza na majaribio ya magari 300 lakini pia tulienda mbali zaidi na kufanya majaribio kwenye magari ya kiwanda Cha Dangote 350 na kufikia zaidi ya magari  600 na hatujaishia hapo tuna mpango wa kuongeza zaidi na kuhakikisha Kila mwananchi anatumia mfumo huo.

“Wengi bado hawaelewi umuhimu wa kutumia gesi kwenye magari,Kuna Faida Sana kwani kunaondoa usumbufu wa gharama za mafuta,Kila gari Ina uwezo wa kutumia gesi kinachotakiwa ni kubadilisha mfumo wa injini ya gari kuwezesha kutumia gesi,”amesisitiza.