October 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mahakama yawapiga kalenda viongozi 20 wa CHADEMA

Na Nathaniel Limu, TimesMajira Online, Singida

KESI  inayowakabili viongozi 20 wa CHADEMA mkoani Singida imeendelea kupingwa kalenda baada ya leo kuahirishwa hadi Novemba 17, mwaka huu ambapo Mahakama ya Hakimu Mkazi itakapotoa uamuzi wa ama kutoa dhamana au la.

Kesi hiyo ambayo ilikuja jana  kwa ajili ya kutajwa,wakili wa washitakiwa hao kutoka Mhyellah and  Advocates ya Arusha mjini, Emmanuel Makiya, aliwasilisha ombi la kuomba dhamana  kwa ajili ya wateja wake.

Hata hivyo,mwanasheria wa serikali Michael Ng’hoboko akisaidiwa na Almachius Bagenda,alisema kuwa kesi hiyo ni kesi ya uhujumu uchumi  ambayo mahakama hiyo haina mamlaka ya kuisikiliza wala kutoa dhamana.

“Kupitia  sheria ya uhujumu uchumi sura ya 200 marejeo ya mwaka 2019 kifungu cha 29 (4) (a),mahakama hii,haina mamlaka ya kusikiliza wala kutoa dhamana,”amesisitiza Wakili Ng’hoboko.

Baada ya mvutano mkali wa hoja za kisheria kati ya wakili wa wateja na waendesha mashitaka, hakimu mwandamizi mahakama ya hakimu mkazi mjini hapa,Cosolanta Singano,aliahirisha kesi hiyo hadi Novemba 17 mwaka huu,atakapotoa maamuzi juu ya dhamana.

Watuhumiwa  ambao ni viongozi wa ngazi mbalimbali ndani ya CHADEMA,ni Emmanuel Simon Lissu (32),Wilson Luta Kidaghoo (59),Gideon Samwel Murya (34),Steven Yesaya Mangu (40),Mika Yesaya Muna ((48),Joseph Herman Daffi (64), Swalehe Ally Mangu (64),Morinyo Mohamed Muhanja (32) na Benedict John (35).

Wengine ni Salum Said Kiduka (34),Ibrahimu Madaraka (21),Juma Hamisi Hisu (31),Lightines Isah Masoud (49),Mashavu Said Ibrahimu (490,Ester Mack Kiwali (48),Debora Shaban (22),Bahati Philemon Sambaa (23),Christina Samwel Hamisi (61) na Noel Sebastian Lemoyani (28).

Jana mahakama hiyo ilifurika wasikilizaji ambao wengi wao walikuwa wanachama wa CHADEMA na kulikuwa na ulinzi wa mkali wa jeshi la polisi.