October 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Lazzaro Mambosasa

Polisi yabaini vurugu za kupinga matokeo ya uchaguzi

Na Penina Malundo, TimesMajira Online, Dar es Salaam

KAMANDA wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Lazzaro Mambosasa, amesema Jeshi hilo limebaini uwepo wa vikundi  vya watu wanaofanya vikao vya siri kupanga njama za kuvuruga kutangazwa kwa matokeo ya uchaguzi.

Hayo ameyasema leo wakati Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), ikiendelea kutangaza matokeo ya kiti cha Urais katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC), na kuongeza kuwa  Polisi wamejipanga kila kona ya jiji hilo, kuhakikisha wanadhibiti vikundi ambavyo vimepanga kuingia barabarani kufanya maandamano.

“Tumebaini uwepo wa vikundi vya watu wanaopanga kuingilia matokeo ya uchaguzi yanayoendelea kutangazwa na NEC, wanahamasisha vurugu na maandamano,” amesema na kuongeza

“Kufanya hivyo ni sawa na kuchezea Demokrasia nchini ambayo kimsingi ni maamuzi ya wananchi, hivyo ni budi kwa wanasiasa mbalimbali kukubaliana na matokeo ya uchaguzi na kujipanga kwa uchaguzi wa mwaka 2025,”amesema

Aidha amesema jeshi hilo limejipanga vyema kuhakikisha halitoi nafasi ya kufanyika kwa aina yoyote ya vurugu ama maandamano kufuatia matokeo ya uchaguzi wa mwaka huu.

“Naomba  wananchi mtoe taarifa kwa Vyombo vya Ulinzi na Usalama, pindi mtakapobaini uwepo wa vikundi vya namna hiyo ili vidhibitiwe mapema,tumejipanga kuhakikisha yeyote anayetaka kuleta vurugu anakutana na mkono wa vyombo vya dola,”amesema