September 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watendaji TAWA wahimizwa kufanya kazi kwa bidii

Na Mwandishi Wetu,TimesMajira Online Tabora

NAIBU Kamishna wa Uhifadhi (Utalii na Huduma za Biashara) wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), Imani Nkuwi amewataka wafanyakazi wa mamlaka hiyo kufanya kazi kwa uzalendo, ueledi na kudumisha upendo miongoni mwao ili kuiwezesha TAWA, kufikia malengo yake waliyokusudia.

Nkuwi ametoa wito huo wakati akiwa katika ziara ya kikazi mkoani Tabora na kufanya mazungumzo na watumishi wa vituo vilivyo chini ya TAWA vilivyopo mkoani hapa.

Vituo hivyo ni Kanda Dhidi ya Ujangili ya Magharibi (KDU), Pori la Akiba la Ugalla, Pori la Akiba Luganzo Tongwe na Pori la Akiba Wembere.

Katika ziara hiyo, Nkuwi ametoa ufafanuzi kwa watumishi hao kuhusu mabadiliko mbalimbali yaliyofanywa na serikali katika shirika pamoja na kusikiliza changamoto zinazowakibili watumishi kwenye vituo vyao.

Naibu Kamishna huyo amewataka watumishi kuzingatia tunu za TAWA, zilizoanishwa katika mpango mkakati wa TAWA kwenye kutekeleza majukumu yao.