Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online, Mbeya
HALMASHAURI ya Wilaya ya Mbeya imetenga kiasi cha sh.milioni 80 mwaka wa fedha 2026/2027 kwa ajili ya ujenzi wa stendi mpya ya kisasa ya maegesho ya malori katika Bonde la Songwe, ikiwa ni jitihada za kuondoa maegesho holela yanayohatarisha usalama wa watumiaji wa barabara katika Mji wa Mbalizi.
Hatua hiyo inakuja kufuatia ongezeko la malori yanayoegeshwa kiholela kando ya barabara kuu, hali inayosababisha ufinyu,msongamano wa magari na kuhatarisha usalama wa wananchi pamoja na watumiaji wengine wa miundombinu hiyo.

Akizungumza Juni 24, 2026 wakati wa kikao cha Baraza la Madiwani cha halmshauri hiyo,kilichojadili hoja za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa mwaka wa fedha unaoishia Juni 30, 2025, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Aida Haule, amesema mradi huo utasaidia kuondoa adha inayowakabili wananchi kutokana na malori kuegeshwa hovyo katika maeneo yasiyo rasmi.
Haule amesema maegesho hayo yamekuwa yakisababisha usumbufu kwa watumiaji wa barabara, wakiwemo madereva wa vyombo vingine vya moto na watembea kwa miguu, huku wakati mwingine yakichangia kutokea kwa ajali za barabarani.
Amesema utekelezaji wa mradi huo unatokana na maelekezo ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya,Beno Malisa, ambaye aliitaka halmashauri hiyo kuweka mkakati wa kudumu wa kudhibiti msongamano wa malori katika eneo la Mbalizi.
Kwa upande wake,Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Beno Malisa amesema, maegesho holela ya malori yamekuwa yakileta usumbufu kwa watumiaji wa barabara na wakati mwingine kusababisha ajali kutokana na kuziba muonekano wa baadhi ya maeneo muhimu ya barabara.
Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya,Erica Yegela, amesema halmashauri imetenga eneo lenye ukubwa wa zaidi ya ekari saba katika Bonde la Songwe ambapo stendi hiyo itajengwa.
Amesema stendi hiyo itakuwa na uwezo wa kuhudumia zaidi ya malori 80 kwa siku, hatua itakayomaliza changamoto ya maegesho holela katika Mji wa Mbalizi na wakati huo huo kuongeza mapato ya halmashauri kupitia ushuru wa maegesho.
Yegela ameongeza kuwa mradi huo ni sehemu ya mikakati ya kuboresha usalama wa barabara, kuimarisha mazingira ya biashara na kuongeza ufanisi katika usimamizi wa usafirishaji wa mizigo ndani ya wilaya hiyo.



More Stories
MD Twange atoa onyo kwa wezi wa miundombinu ya umeme
WRRB yaanza uimarishaji mfumo stakabadhi za ghala
Senyamule:Serikali inapaswa kuzitambua Kampuni zinazofanya biashara ya ardhi